OFISI ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali imetakiwa kuweka sheria za nchi mitandaoni ili wananchi waweze kuzisoma na kuzielewa kwa urahisi. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Ombi hilo limetolewa leo tarehe 6 Februari 2019 jijini Dar es Salaam na Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma wakati akizungumza kwenye kilele cha maadhimisho ya wiki ya sheria nchini.
“…Ombi kwa mpiga chapa wa serikali aweke sheria zote za Tanzania mitandaoni, ili mwananchi aweze kujua sheria na kujua utaratibu maalumu wa kufuatilia haki zake mahakamani,” amesema Prof. Juma.
Katika hatua nyingine, Prof. Juma amesema mahakama imedhamiria kuboresha matumizi ya Teknolojia, Habari na Mwasiliano (TEHAMA) katika utoaji haki ili kurahisisha usimamizi wa mashauri.
“Katika matumizi ya TEHAMA ya utoaji haki, mahakama imetoka kwenye mfumo wa nadharia na kwenda kwa vitendo, unawezesha kufanyika kwa urahisi mambo mbalimbali ya kusimamia mashauri, kufungua mashauri, kuitwa mashaurini na wananchi kusoma hukumu za mashauri zilizotolewa,” amesema Prof. Juma.
Katika maadhimisho hayo yaliyobeba kauli mbiu ya ‘Utoaji haki kwa wakati ni jukumu la mahakama na wadau’, kulifanyika uzinduzi wa huduma ya mahakama inayotembea pamoja na mfumo wa kilektroniki wa kuratibu mashauri.
Leave a comment