HATUTAFUMBIA macho watu, taasisi na vyama vya siasa vitakavyokiuka sheria. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 1 Oktoba 2019 na Benedict Wakulyamba, Kamishna wa Polisi wakati akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Simon Sirro.
Kamishna Wakulyamba alikuwa kwenye semina ya Makamanda wa Jeshi la Polisi wa Mikoa ya Tanzania Bara na Visiwani.
Kamanda Wakulyamba amesema, kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa, jeshi hilo limejipanga vyema kusimamia uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika Novemba mwaka huu.
Amesema, jeshi hilo halitakuwa radhi kuona mtu, taasisi au kikundi chochote kinafanya ndivyo sivyo kwenye uchaguzi huo.
“Sisi kama Jeshi la Polisi hatujaanza leo na wala hatutaacha kujipanga kikamilifu kuhakikisha shughuli hii ya uchaguzi inafanyika kwa Amani, ili kazi za serikali ziendelee bila bughudha yoyote,” amesema Kamanda Wakulyamba.
Kamanda Wakulyamba amewataka Wananchi na makundi yanayohusika na uchaguzi, kushiriki katika zoezi kwa kufuata katiba na sheria za nchi.
“Kwa niaba ya IGP, wito wetu kwa wananchi na makundi yanayohusika na uchaguzi kuwa wanashiriki zoezi hilo kwa kufuata misingi. Vyombo vinavyosimamia uchaguzi wajibu wao ni kuhakikisha suala la uchaguzi linakwenda vizuri.
Jamii pia ina jukumu la kusimamia uchaguzi unakwenda vizuri. Polisi nao wana wajibu wa kusimamia uchaguzi na kuhakikisha unakuwa mzuri,” ,” amesema Kamanda Wakulyamba na kuongeza;
“Suala la uchaguzi ni la kisiasa. Hivyo lazima lisimamiwe kwa kufuata misingi yote ya kisiasa. Ni wajibu wa kila mmoja kujua kuwa upo mfumo wa kisiasa tunaoutumia kupata viongozi wetu,” amesema Wakulyamba ambaye ni Kamishna wa Polisi, Utawala na Menejimenti ya Rasilimali Watu.
Leave a comment