SERIKALI imewafutia kesi ya uhujumu uchumi namba 1 ya mwaka 2019 Askari Polisi nane, waliokuwa wanatuhumiwa kutorosha shehena ya madini ya dhahabu Jijini Mwanza. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hayo amesema Biswalo Mganga, Mkurugenzi wa Mashtaka Tanzania (DPP) wakati akizungumza na wanahabari leo tarehe 17 Julai 2019.
DPP Mganga amesema, baada ya kuifuta kesi hiyo, mamlaka husika ziko katika utaratibu wa kuwarejesha kazini polisi hao.
Polisi hao ni pamoja na Morice Okinda, Mkuu wa Operesheni mkoani Mwanza, F 1331 PL Matete, G 5080 D/C Maingu, G 6885 D/C Alex, G 1876 D/C Japhet, G 7244 D/C Timothy na E 6948 D/C PL Kasala.
DPP Mganga ameeleza kuwa, ameamua kuwafutia mashitala polisi hao, kwa sababu ya kulinda masilahi ya taifa.
Mnamo tarehe 11 Januari mwaka huu, polisi hao pamoja na wafanyabiashara wanne, walifikishwa katika mahakama jijini Mwanza, wakikabiliwa na mashitaka matano.
Polisi hao walidaiwa kufanya makosa katika nyakati tofauti, kati ya tarehe 4 na 5 mwezi Januari 2019.
Miongoni mwa mashitaka yaliyokuwa yanawakabili ni pamoja na, uhujumu uchumi, kula njama za kupanga uhalifu na utakatishaji fedha.
Sakata hili liliibuka mwanzoni mwa mwezi Januari mwaka huu, ambapo Rais John Magufuli aliagiza mamlaka husika kuwachukulia hatua polisi hao, ikiwemo kuwahoji kuhusu tuhuma zinazowakabili.
Awali, Polisi hao walituhumiwa kisafirisha kinyume na sheria shehena ya madini ya dhahabu pamoja na fedha kiaso cha Sh. 305 Milioni.
Leave a comment