MSEMAJI wa serikali ambaye pia ni mkurugenzi mkuu wa Idara ya Habari (Maelezo, Hassan Abbas ametangaza kibano kwa tasnia ya habari kinachohusu usajili upya wa magazeti, majarida na machapisho yote yaliyopo pamoja na kulipia shilingi milioni moja kama gharama za leseni kwa mwaka, anaandika Jovina Patrick.
Abbas ametangaza maelekezo hayo leo alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam na kwamba mmiliki aliyefuata agizo hilo hataruhusiwa kuchapisha gazeti ama jarida lolote hapa nchini.
Awali gharama hizo za leseni hazikuwapo isipokuwa mmiliki alikuwa anatakiwa kusajili gazeti ama jarida na akishapata usajili anaanza kuchapisha bila malipo mengine.
Akizungumza na waandishi wa habari, Abbas amesema zoezi hilo ni utekelezaji wa matakwa ya kifungu cha 5(e) cha sheria ya huduma za habari, ambayo ni muendelezo wa azma ya waandishi wa habari kuwa na taaluma inayowajibika.
Usajili huo umeanza leo na unatarajia kumalizika Octoba 15, mwaka huu na kwamba baada ya muda huo kumalizika gazeti ama jarida ambalo halikusajiliwa halitaruhusiwa kuchapishwa.
“Gazeti au jarida lolote litakaloshindwa kujisajili na kupata leseni halitaruhusiwa kutoa nakala zake na endapo likitoa nakala litachukuliwa hatua hali za kisheia” anasema Abbas.
Amesema kwa magazeti yaliyopo sasa mwisho wa kusajiliwa upya ni Oktoba 15, mwaka huu, lakini yale yanayotaka kuanzishwa kwa mara ya kwanza usajili wake utaendelea baada ya tarehe hiyo.
Nyaraka zinazohitajika katika usajili huo ni pamoja na sera ya chombo husika, viwango vya elimu kwa Wahariri pamoja na Waandishi wao katika chombo husika.
Leave a comment