SERIKALI imeombwa kuwatambua wafugaji wa Ngamia na kusaidia kuwapunguzia gharama za kuwafuga kwa kuwa wana faida zaidi kuliko wanyama wengine, anaandika Dany Tibason.
Maombi hayo yalitolewa na Ally Kuleva ambaye ni mfugaji wa Ngamia, katika maonesho ya Nanenane mkoani Morogoro.
Kuleva anatokea kijiji cha Kambi ya Kumi wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma.
Amesema wafugaji wengi wa ngamia wanakumbwa na changamoto mbalimbali ikiwamo ukosefu wa dawa za kuwatibia wanyama hao.
Ameongeza kuwa kwa sasa serikali ni kama haijaweza kutambua na kuboresha ufugaji wa Ngamia kwa kuwa haiwapi kipaumbele wafugaji hao kwani mpaka sasa hata katika madawa ya mifugo huwezi kupata dawa ambayo inaweza kuwatibu wanyama hao.
Ametaja faida ya wanyama hao kuwa ni pamoja na maziwa yake kutumika kwa ajili ya kutibu vidonga vya tumbo, shinikizo la damu pamoja na magonjwa mbalimbali.
Aidha, amesema mkojo wa mnyama huyo pia ni dawa inayotibu ugonjwa wa pumu.
Leave a comment