Thursday , 28 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Serikali yanena kuhusu viwanda, uvamizi Zanzibar
Habari za SiasaTangulizi

Serikali yanena kuhusu viwanda, uvamizi Zanzibar

Bunge likiendelea na vikao vyake
Spread the love

SERIKALI ya awamu ya tano imetoa taarifa kuhusu mipango ya utekelezaji wa mambo mbalimbali yanayohusu utendaji wa serikali pamoja na utekelezaji wa Bajeti ya mwaka 2016/2017, anaandika mwandishi wetu.

Hii ndiyo taarifa kamili iliyotolewa na serikali;

 TAARIFA KWA UMMA

SERIKALI YAELEZA UTEKELEZAJI WA MASUALA MBALIMBALI BUNGENI

Dodoma, Jumanne, Januari 31, 2017:

Serikali leo imeainisha utekelezaji na kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya maendeleo kwa wananchi katika sekta mbalimbali katika kikao cha kwanza cha Mkutano wa Sita wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Majibu ya Serikali kwa baadhi ya hoja ni kama ifuatavyo:

Ujenzi Nyumba za Walimu 

Akijibu hoja kuhusu ujenzi wa nyumba za walimu, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Selemani Jafo, ameliambia Bunge kuwa Serikali ilitenga kiasi cha Sh. Bilioni 13.9 katika Bajeti ya mwaka huu kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu wa Sekondari, na Shilingi bilioni 11.4 kwa nyumba za walimu wa Shule za Msingi.

Aidha, Waziri Jafo ameeleza kuwa tayari nyumba 146 za walimu zimeshajengwa nchini kupitia Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari.

Pia amezungumzia Serikali kuanza kulipa madeni ya walimu.

Ujenzi wa Viwanda Nchini

Akijibu swali kuhusu uwekezaji wa viwanda nchini hususani mkoani Tabora ambako kuna kilimo cha Tumbaku na maeneo mengine yenye malighafi, Mhandisi Edwin Ngonyani kwa niaba ya Waziri wa Viwanda ameliambia Bunge kuwa tayari Serikali imeshafanya mazungumzo na wawekezaji kutoka Vietnam na kuzitaka Halmashauri zote nchini kuendelea kuitikia wito wa kutenga maeneo ya uwekezaji.

“Kituo cha uwekezaji Nchini (TIC) kimepewa maelekezo maalum kunadi fursa hii kwa wawekezaji katika sekta ya tumbaku na sigara hapa nchini,” alisema Mhandisi Ngonyani ambaye pia ni Naibu Waziri, Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Tupende Bidhaa Zetu

Akijibu hoja kuhusu bidhaa nyingi za Kenya kuingia nchini, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Suzan Kolimba amesema moja ya changamoto inazozikumba bidhaa za Tanzania ni wananchi wake kupenda vya nje.

“Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali iliunda Kamati ya Kitaifa ya Kudhibiti na Kusimamia Uondoaji wa wa Vikwazo visivyo vya Kiforodha na kuhamasisha wafanyabiashara nchini kuzalisha bidhaa zenye ubora,” alisema.

Serikali yagharamia 100% umeme vijijini

Serikali imesisitiza kuwa inagharamia ujenzi wa umeme vijijini kupitia Wakala wa Kusambaza Umeme Vijijini (REA) kwa asilimia 100. Akijibu maswali ya wabunge, Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani, alisema wananchi wanalazimika kuchangia Sh. 27,000 tu ambazo ni gharama za kodi ili waunganishiwe huduma hiyo wakati mradi ukiwa unaendelea.

“Lengo ni kuhamasisha na kuwawezesha wananchi wa vijijini wenye vipato vidogo kuweza kupata huduma za umeme kwa gharama nafuu,” alisema akisisitiza kuwa wale ambao huomba huduma hiyo baada ya wataalam wa REA kumaliza kazi yao ndio hulazimika kulipia umeme huo kwa Sh. 177,000 tu badala ya Sh. 320,960/wanazotozwa wakazi wa mijini kwa umbali usiohitaji nguzo.

Bei ya maji kupungua

Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhandisi Gerson Lwenge amesema Serikali itaendelea kupunguza gharama za maji nchini hasa vijijini kadiri gharama za umeme zitakavyoendelea kupungua hasa wakati huu nchi inapoingia katika uchumi wa gesi.

Aliongeza kuwa kwa upande wa vijijini miradi ya umeme wa jua na nishati nyingine za bei nafuu pia itasaidia kupunguza gharama za umeme na kusaidia wananchi kupata maji katika miradi mingi inayondelea sasa nchini.

Madai ya Unyanyasaji Zanzibar

Serikali imewataka wananchi wote wanaodai kufanyiwa unyanyasaji na vikosi vya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kutoa taarifa za matukio hayo polisi ili hatua stahiki zichukuliwe.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba alisema kwa kuwa hakuna tarifa za kuripotiwa kwa matukio hayo katika kituo chochote cha Polisi, atachukua pia hatua za kutuma maafisa wake kufanya uchunguzi zaidi.

 Imetolewa na:

Dkt. Hassan Abbasi,

Mkurugenzi Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali.

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

Habari za SiasaTangulizi

Mashirika matano yapata hasara mabilioni ya fedha

Spread the loveMASHIRIKA matano ya Serikali yanayojiendesha kibiashara, yamepata hasara ya mabilioni...

Habari za SiasaTangulizi

CAG aibua madudu halmashauri 10, TANESCO na MSD

Spread the loveRIPOTI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali...

error: Content is protected !!