SERIKALI imekanusha taarifa zinazosambaa mitandaoni kwamba kuna mlipuko wa virusi vya ugonjwa wa Ebola hapa nchini. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Hivi karibuni zimeibuka taarifa za uwepo wa Ebola hapa nchini katika mitandao ya kijamii, zinazodai kwamba kuna watu wawili wamefariki dunia kutokana na ugonjwa huo.
Akitoa ufafanuzi kuhusu suala hilo, Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto amesema taarifa hizo si za kweli na kwamba hakuna mgonjwa aliyethibitika kuwa na Ebola.
“Wizara inaendelea tena kusisitiza kuwa hadi sasa hakuna mgonjwa yeyote aliyethibishwa kuwa na ugonjwa huu. Hivyo kwa sasa hakuna ugonjwa wa Ebola nchini,” amefafanua Waziri Ummy.
Kuhusu watu wawili wanaodaiwa kupoteza maisha kwa sababu ya kuathirika na Ebola, Waziri Ummy amesema wizara yake imechukua sampuli za marehemu hao na kuzifanyia uchunguzi ambapo imebainika kwamba hawakuwa na ugonjwa huo.
“Uvumi wa kuwepo ugonjwa huu nchini ni kutokana na kuwepo kwa taarifa za watu wawili wa ugonjwa huu, Wizara imechukua sampuli na kujiridhisha kuwa walikuwa hawana virusi vya Ebola. Hivyo kwa sasa hakuna ugonjwa wa Ebola nchini,” amesisitiza Waziri Ummy.
Aidha, Waziri Ummy amewatoa hofu Watanzania na kuwaonya watu wanaoeneza taarifa potofu juu ya ugonjwa huo, akisema kwamba mwenye dhamana ya kufanya hivyo ni Waziri anayeshughulika na masuala ya afya.
Leave a comment