Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Serikali yajikanyaga mbele ya wahisani
Habari za SiasaTangulizi

Serikali yajikanyaga mbele ya wahisani

Spread the love

SERIKALI imekana madai ya nchi wahisani juu ya kuwapo kwa vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu, mauaji, utesaji na uvunjifu wa demokrasia nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).

Hata hivyo, taarifa ya serikali iliyotolewa na wizara ya mambo ya nchi za nje na uhusiano wa kimataifa, Ijumaa iliyopita, imeshindwa kujibu madai kuwa “Tanzania siyo tena eneo salama kwa watetezi wa haki za binadamu na wakosoaji wa sera za serikali.”

Badala yake, serikali inaituhumu mabalozi kwa kile walichoita, “kukalia kimya masuala mazito ambayo Tanzania imepitia huko nyuma.”

Inasema, “ni jambo la kawaida kwa wanadiplomasia wa kigeni kufuatilia na kuripoti hali ya kisiasa na usalama inayoendelea katika nchi walizotumwa.

“Lakini tunashangazwa na ukimya uliowazi katika kipindi cha nyuma wa mabalozi hawa juu ya vitisho vya uvunjifu wa amani uliokuwa haujawahi kutokea na changamoto nyingine ambazo Tanzania imekuwa ikikabiliana nazo katika maeneo matatu ya Kibiti-Mkuranga –Rufiji yanayopakana.”

Hatua ya serikali kujibu tuhuma za mabalozi imefuatia matamko yaliyotolewa na nchi za Magharibi wiki mbili zilizopita, yakielezea wasiwasi wao kuhusiana na matukio ya kiusalama yanayoendelea kutikisa nchi.

Miongoni mwa matukio hayo, ni shambulio la risasi dhidi ya mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu na mauaji ya mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Chuo cha Usafirishaji cha taifa (NIT), Akwilina Akwiline.

Lissu alinusurika kifo baada ya kushambuliwa kwa risasi na wanaoitwa na serikali, “watu wasiofahamika,” wiki mbili baada ya kunukuliwa akisema, “maisha yangu yako hatarini.”

Lissu ambaye pia ni Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Mnadhimu wa Kambi rasmi ya upinzani bungeni, mwanasheria mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo, alishambuliwa kwa risasi za moto majira ya saa saba na nusu mchana, tarehe 7 Septemba mwaka jana.

Shambulio dhidi ya Lissu, lilifanyika nje ya nyumba yake, Area D, mjini Dodoma. Alikuwa akirejea nyumbani kutokea bungeni.

Naye Akwiline, aliuawa kwa kupigwa risasi na jeshi la polisi, maeneo ya Mkwajuni, jijini Dar es Salaam. Alikuwa akitokea shuleni kwake Mabibo, kuelekea Bagamoyo alikokuwa anakwenda kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo.

Polisi walidai kuwa walilazimika kufyetua risasi ili kukabialiana na wafuasi wa Chadema, waliokuwa wakielekea ofisi ya mkurugenzi wa manispaa ya Kinodoni, Aron Kagurumjuli, ili kumshinikiza kutoa hati za viapo kwa mawakala wake, waliokuwa wanasimamia uchaguzi mdogo wa jimbo la Kinondoni.

Matukio mengine yaliyosababisha Umoja wa Ulaya (EU) na Marekani, kushinikiza serikali ya Tanzania, ni kupotea kwa mwandishi wa habari, Azory Gwanda na kutekwa na kuuawa kwa kada wa Chadema, Daniel John.

Kada huyo ambaye alikuwa katibu wa Kata ya Hananasifu, jimbo la Kinondoni, alitoweka akiwa na Reginald Mallya aliyejikuta akiwa ametupwa ufukweni mwa bahari, akiwa na jeraha la panga kichwani na akiwa amevunjika mkono.

Mwili wa John ukikutwa hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), ukiwa na michubuko; jeraha la panga kichwani na upande mmoja wa kichwa umebonyea kuashiria alipigwa na kitu kizito. John alikutwa na mauti kipindi cha uchaguzi mdogo wa ubunge katika jimbo la Kinondoni.

Kwa upande wa Azory Gwanda, aliyepotea tarehe 21 Novemba 2017 baada ya kuchukuliwa nyumbani kwake, maeneo ya Kibiti, mkoani Pwani, na watu waliojitambulisha kuwa “maofisa wa usalama,” mpaka sasa hajulikani alipo.

Mwandishi huyo wa habari aliyekuwa akiripoti taarifa za matukio ya Kibiti, anadaiwa kuwa waliomchukua nyumbani kwake, walitumia gari aina ya Land Cruiser.

Kwa mujibu wa serikali, tamko hilo halikuzingatia mashambulizi ya silaha yaliyotokea mkoani Pwani.

Aidha, serikali inasema, matamko yaliyotolewa na mabalozi, hayakutambua uhusiano uliokuwepo kati ya hatua za kishujaa ambazo zimechukuliwa na Rais Magufuli kuondoa ufisadi, madawa ya kulevya, ukwepaji kodi, ujangili wa nyara za serikali na kuhakikisha uwajibikaji katika sekta binafsi na za umma, na matukio ya usalama.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Wabunge waikalia kooni TAKUKURU Bungeni

Spread the love  BAADHI ya wabunge wamelia na changamoto za utendaji wa...

Habari za SiasaTangulizi

Mpina ataka Waziri Majaliwa ajiuzulu, akosoa teuzi za mawaziri

Spread the love  MBUNGE wa Kisesa, Luhaga Mpina, amemtaka Waziri Mkuu, Kassim...

Habari za Siasa

CCM yakemea ufisadi, yaipa kibarua TAKUKURU

Spread the love  CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimekemea vitendo vya ubadhirifu wa...

Habari za Siasa

Bajeti ya Ikulu 2024/25 kuongezeka, bunge laombwa kurudhia Sh. 1.1 trilioni

Spread the love  WIZARA ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa...

error: Content is protected !!