SERIKALI imetoa siku nne kwa wanunuzi takribani 35 waliojitokeza kununua korosho, kupeleka barua katika Ofisi ya Waziri Mkuu inayoonesha kiasi cha tani wanazohitaji na siku watakazozichukua. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Agizo hilo limetolewa leo tarehe 9 Novemba 2018 jijini Dodoma na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati akitoa tamko la serikali kuhusu ununuzi wa zao la korosho.
Majaliwa ameeleza kuwa, siku hizo zikipita bila ya wanunuzi hao kutekeleza agizo hilo, serikali italazimika kufuta usajili kwa wote waliojisajili kununua zao hilo.
“Mwenye nia ahakikishe katika siku hizo nne iwe ndio mwisho wa kununua korosho, na waandike barua kwani ofisi yangu ipo wazi saa 24 wana nafasi ya kuleta barua wakati wowote wakionesha nia yao na kiwango wanachokihitaji, zaidi ya hapo serikali haitoruhusu kampuni yoyote kununua korosho tena,” amesema Majaliwa.
Majliwa amesema wakati Rais John Magufuli alipozungumza na wanunuzi wa korosho walikubaliana kununua zao hilo kwa bei inayoanzia Sh. 3,000 na kuendelea, na kwamba baada ya kikao hicho ununuzi katika minada imeendelea kusuasua na tani zilizonunuliwa zilikuwa kidogo sana.
Amesema hali hiyo ni kama mgomo baridi kitendo ambacho si sawa kwani malengo ya serikali na sekta binafsi ni kumfanya mkulima apate bei nzuri.
“Hali hii haifurahishi kwa sababu serikali imedhamiria kuboresha mazao yanayolimwa na wakulima kwa kuwasaidia kuanzia katika hatua za utayarishaji wa mashamba, upatikanaji wa pembejeo na masoko ili waweze kunufaika na kilimo na kupata tija katika mazao hayo,” amesema Majaliwa.
Leave a comment