MBUNGE wa Igalula Musa Ntimizi (CCM) ameihoji serikali sababu ya kutozisajili shule shikizi zilizojengwa karibu na makazi ya wananchi, anaandika Dany Tibason.
Akiuliza swali la msingi bungeni leo, Ntimizi amesema serikali imekuwa ikihamasisha ujenzi wa shule nyingi zaidi karibu na makazi ya wananchi yaani ‘satelite schools’ kupitia wabunge na madiwani.
“Sasa wananchi wameitikia wito na viongozi tumezichangia sana, Je kwanini serikali haisajili shule hizo na kupeleka walimu?” amehoji Ntimizi
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhandisi Stellah Manyanya amesema lengo la kuanzishwa kwa shule hizo ni kuwezesha watoto wadogo wa darasa la kwanza hadi darasa la tatu ambao hawana uwezo wa kutembea umbali mrefu kufuata shule mama kusoma karibu na makazi yao.
Aidha amesema sababu ya kutosajiliwa shule hizo na kupangiwa walimu ni kutokana na shule hizo kuwa za muda mfupi ambazo zipo chini ya shule mama husika.
“Mfano ikianzishwa kwa sababu ya mafuriko, yakiisha shule hiyo pia inakufa, vile vile shule hizi hazikidhi vigezo vya kusajiliwa ambavyo ni uwepo wa ofisi ya mwalimu mkuu, mwalimu mkuu msaidizi, ofisi za walimu, vyoo, vyumba vya madarasa, maktaba na stoo,” amesema Mhandisi Manyanya
Akiuliza swali la nyongeza Ntimizi ametaka kujua serikali inasema nini kuhusu watoto wa kike wanaotembea umbali mrefu wa zaidi ya kilomita 40 kwenda shule na kurudi nyumbani hali inayosababisha watoto wa kike kupata mimba na wavulana kutokana umuhimu wa kusoma.
Pia alitaka kujua serikali inasema nini juu ya shule nyingi ambazo zimejengwa na zimekidhi vigezo kwa asilimia 80 lakini hazijasaliwa.
Akijibu swali hilo, Mhandisi Manyanya amesema shule zinapojengwa kinapaswa kuwe na ushirikishwaji lakini pia zinapaswa kujengwa katika maeneo ambayo ni rasmi na isiwe imejengwa kwa sababu fulani.
Hata hivyo amesema shule ambazo zimekidhi vigezo kwa zaidi ya asilimia 80 wahusika wafuate taratibu za usajili ili shule hizo ziweze kusajiliwa.
Leave a comment