SERIKALI, iko mbioni kuvirejesha serikalini viwanda vyake vinane vilivyokuwa vinaendeshwa na wawekezaji, anaandika Dany Tibason.
Taarifa hiyo ilitolewa bungeni jana na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, alipokuwa akiwasilisha bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2017/18.
“Ofisi ya Msajili wa Hazina, ilifanya ufuatiliaji na tathmini kwenye taasisi na mashirika ya umma 72 yaliyobinafsishwa kwa lengo la kukagua ufanisi na kuhakiki utekelezaji wa masharti ya mikataba ya mauzo.
“Matokeo ya ufuatiliaji huo pamoja na mambo mengine, yameonyesha wamiliki wa viwanda vinane, wamekiuka masharti ya mikataba ya mauzo na kutoonyesha nia ya dhati ya kuvifufua.
“Viwanda hivyo ni pamoja na Tembo Chip Board, National Steel Corporation, Mang’ula Mechanical & Machine Tools, Mkata Sawmills, Tanganyika Packers Shinyanga, Kiwanda cha Korosho Lindi, Kiwanda cha Korosho Newala na Mgodi wa Pugu Kaolin.
“Hatua za kisheria dhidi ya wamiliki hao zinafanyika katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kabla ya kuendelea na hatua zaidi ikiwamo kuvirejesha chini ya umiliki wa Serikali.
“Aidha, baada ya ufuatiliaji huo, Ofisi ya Msajili wa Hazina imechukua hatua mbalimbali kwa mashirika na viwanda vingine vinavyosuasua zikiwamo kuwataka wawekezaji kuongeza uzalishaji,” amesema Dk. Mpango.
Akizungumzia Kampuni ya Usafiri Dar es Salaam (UDART), Dk Mpango amesema usafiri huo umezidi kuimarika baada idadi ya abiria kuongezeka kutoka 76,000 kwa siku mwezi Mei mwaka jana hadi kufikia abiria 180,909 kwa siku Mwezi Machi mwaka huu.
“Baadhi ya safari kama vile kutoka Kimara hadi Kivukoni, muda wake wa msongamano mkali umepungua kutoka masaa mawili hadi dakika 40 na ajira mpya zaidi ya 1,000 zimezalishwa zikihusisha madereva, mafundi karakana, walinzi pamoja na wahudumu,” amesema Dk. Mpango.
Leave a comment