PROFESA Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, amesema Serikali imejipanga kuandaa na kutoa mafunzo ya uwezeshaji wa programu za kisomo na kufanya kampeni kwa kanda za kitaaluma ili watu waelewe kazi za Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima. Anaripoti Khalifa Abdallah … (endelea).
Ndalichako amesema hayo wakati akizindua Bodi ya Wakurugenzi ya Taasisi hiyo ambayo baadhi ya watu wakiwemo wabunge bungeni walikuwa wakishinikiza ifutwe kufuatia kutokuwa na ufahamu wa majukumu ambayo taasisi hiyo inafanya.
“Watu wamekuwa wanauliza kuwa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima inafanya nini lazima tufanye kampeni ya kisomo ili muonekane, watu wajue mnafanya nini na waweze kuja kujiunga,” amesema.
Profesa Ndalichako amesema kuwa imani yake ni kuwa Bodi hiyo mpya kwa kushirikina na Menejimenti ya Taasisi hiyo itaweza kupunguza idadi ya watu wasiojua kusoma na kuandika.
Kwa mujibu wa Sensa ya mwaka 2012 idadi ya wasiojua kusoma na kuandika imekuwa ni asilimia 22 ambayo Waziri Ndalichako amesema idadi hiyo ilikuwa kubwa hivyo ipungue.
Naye Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Wakurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima, Naomi Katunzi amesema anamshukuru Rais Magufuli kwa kumuamini kumpa nafasi hiyo na kuwa pamoja na nafasi mbalimbali alizowahi kushika katika serikali ya Tanzania lakini amebobea kwenye masuala ya mitaala hivyo kitendo cha Rais kumteua kuwa Mkurugenzi wa Bodi hiyo ambayo mitaala imezungumzwa kwa kiasi kikubwa ni kama amerudishwa nyumbani.
Amesema atahakikisha anaisimamia taasisi hiyo ipasavyo kama matakwa ya serikali ilivyotaka ili kuhakikisha idadi hiyo ya wasiojua kusoma na kuandika inapungua.
Leave a comment