Thursday , 25 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Sakata la ATCL: TLS yamvaa Musiba
Habari za SiasaTangulizi

Sakata la ATCL: TLS yamvaa Musiba

Spread the love

CHAMA cha Mawakili Tanzania Bara (TLS), kimelaani shutuma zinazoelekezwa kwa mawakili kwamba hawana uzalendo, wakihusishwa na kukamatwa kwa ndege ya Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) nchini Afrika Kusini. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).

Katika tamko lake ililolitoa leo tarehe 28 Agosti 2019, TLS imeeleza, kazi ya utetezi ni miongoni mwa hatua za kuifia haki ambayo kila mmoja anaihitaji.

Tamko hilo linatolewa huku Cryspian Musiba, anaejitambulisha kuwa mwanahaharakati na mtetezi wa Rais John Magufuli, akituhumu wanasheria na mawakili, kwamba wanahusika katika kushawishi na kuibua kesi iliyosababisha ndege hiyo kukamatwa.

Musiba anasema, mawakili na wanasheria wasio wazalendo wamekuwa wakishirikiana na wanasiasa kushinikiza wenye madeni na Tanzania kuibua madeni hayo, jambo ambalo linampa wakati mgumu Rais Magufuli.

“Haijawahikutokea raia wa Marekani kushirikiana na mtu wa nje kusaliti taifa lake…, kuna baadhi ya wapumbavu wachache na wajinga wachache wanakwenda nje kushawishi wale wote wenye kesi na madeni na Tanzania waingize kwenye kesi,” amesema Musiba.

TLS imesema, kumekuwa na tuhuma zinazoelekwa kwa mawakili Watanzania kutokuwa wazalendo, na kwamba ndio waliosababisha ndege hiyo kukamatwa nchini Afrika Kusini.

Taarifa hizo ambazo zimeibua mjadala wa uzalendo kwenye mitandao ya kijamii na kuandikwa leo tarehe 28 Agosti 2019 kwenye gazeti la Tanzanite linalomilikiwa na Cryspian Musiba, anayejitambulisha kuwa mtetezi wa Rais John Magufuli, zimetuhumu mawakili wa Tanzania kukosa uzalendo.

Ndege hiyo aina ya Airbus A220-300, imezuiwa kuondoka Afrika Kusini kwa amri ya mahakama kuu ya Gauteng, jijini Jonesburg kutokana na kushindwa kulipa deni la mdai ambaye ametambulishwa kuwa mkulima.

Dk. Leonard Chamuriho, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano alitoa taarifa ya kukamatwa ndege hiyo tarehe 23 Agosti 2019.

“Katika siku za hivi karibuni, kumekuwa na matukio yanayoashiria kubeza na kutuhumu taaluma ya uwakili kwa vigezo mbalimbali ikiwemo tuhuma za ukosefu wa uzalendo dhidi ya mawakili.

“Pia kumekuwa na matukio ya kutotoa heshima stahiki kwa taaluma na wanataluuma wa sheria kwa kukamatwa na kuwatuhumu pamoja na wateja wanaowahudumia, kuwadhihasha na kuhamasisha uvunjifu wa sheria za nchi kwa makusudi, vitendo ambavyo vinafanywa na kuchochewa na watu mbalimbali wakiwemo watumishi na viongozi wa serikali na wale wanaojifanya kuwa ni wanaharakati huru,” ameeleza Dk. Rugemeleza Nshala, Rais wa TLS kwenye taarifa ya chama hicho.

Ameeleza, mawakili hawapaswi kutuhumiwa kwamba hawana uzalendo pale wanapotenda kazi yao ya uwakili, na kutekeleza wajibu wao kwa wateja.

“Matamko na vitendo vya kuwatisha, kuwatuhumu na kuwananga mawakili ni ukiukwaji na usiginaji mkubwa wa Katiba na sheria za nchi yetu; misingi ya utawala bora, haki ya mtu au chombo chochote kusikilizwa kabla ya uamuzi kutolewa dhidi yake na ni kiashiria tosha cha uzuiaji wa haki kutendeka,” imelaani taarifa hiyo ya TLS.

Imeeleza, wajibu mkuu wa mawakili ni kutelekeza majukumu yao ya kuhakikisha sheria za nchi zinasimamiwa na kufuatwa ili kuifikia haki.

Tamko hilo limebeba mambo makuu matatu;-

Mosi; limekumbusha umma na viongozi kuwa mawakili wana wajibu kwa mteja au wateja wao wenye shida mbalimbali za kisheria kama vile kuwakilishwa kwenye mashauri jinai na madal ili waifikie haki na kutoa ushauri wa kisheria katika masuala mbalimbali na kujengewa uwezo kupitia elimu ya ufahamu wa sheria.

Maadili ya uwakili yanawataka mawakili kutobagua mteja au wateja na kufanya kazi ya utetezi wa wateja wao kwa uadilifu na ukamilifu ili kuisaidia mahakama na vyombo vingine vyote vya utoaji haki kufikia maamuzi sahihi.

Pili, TLS inakemea na kulaani vitendo vya kuhamasisha uvunjifu wa sheria unaofanywa na mtu mmoja mmoja, makundi, viongozi wa dini, viongozi wa siasa kuwa ni kinyume na misingi ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977.

Tatu; TLS inaendelea kukemea na kulaani vitendo vinavyotweza na kukebehi taaluma ya uwakili nchini. kitendo cha wakili kukamatwa na kuunganishwa pamoja katika kesi inayowakabiii wateja wake ni dhihaka kubwa kwenye taaluma ya uwakili.

Mawakili hao wamewataka wananchi kutobeza mchango na kazi ya taaluma ya mawakili nchini “tunasisitiza kuwa mawakili ni kiungo muhimu cha kufikia haki, kulinda amani na utu!”

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Kilosa yawa mfano wa kuigwa miradi ya Mwenge nchini

Spread the love  KIONGOZI wa Mbio za Mwenge Kitaifa Godfrey Mzava amezitaka...

Habari za SiasaTangulizi

Biteko ataja vipaumbele 7 bajeti nishati 2024/25

Spread the love  NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mwekezaji amwaga bil. 39 kujenga viwanda 3 vya uchenjuaji

Spread the loveKampuni ya Mineral Access System Limited (MAST) inayoiwakilishwa kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

Mpwa wa Magufuli mbaroni kwa kusambaza picha za utupu

Spread the loveJESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewakamata...

error: Content is protected !!