SERIKALI ya Rwanda imeridhishwa na utoaji huduma katika Bandari ya Dar es Salaam nchini Tanzania na kuahidi kuendelea kuitumia bandari hiyo ambayo imekuwa ikihudumia zaidi ya asilimia 80 ya mizigo ya nchi hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa iliyotolewa leo Ijumaa Ijumaa tarehe 18 Desemba 2020 na Baraka Samson, Ofisa Mawasiliano wa Ubalozi wa Rwanda nchini Tanzania imesema, hayo yalisemwa na Balozi wa Rwanda nchini Tanzania, Meja Jenerali Charles Karamba baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof Palamagamba Kabudi jana Alhamisi jijini Dodoma.
Balozi Karamba amesema, Tanzania na Rwanda si nchi jirani pekee, bali ni ndugu wa damu na Rwanda inaiona bandari ya Dar es Salaam kama bandari ya Rwanda.
Katika mazungumzo hayo, Balozi Karamba alitumia fursa hiyo kumfahamisha Profesa Kabudi juu ya uwepo wa mkutano wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Madola (Commonwealth) unaotarajiwa kufanyika Juni mwaka 2021 nchini Rwanda ambapo itakuwa fursa nzuri zaidi kwa wafanyabiashara wa Tanzania na Rwanda kufanya biashara kutokana na uwepo wa mkutano huo.
Naye Profesa Kabudi alieleza Tanzania itaendelea kuweka mazingira mazuri kwa uwekezaji na biashara kwa nchi jirani na nyingine zinaoitegemea Tanzania kupokea na kusafirisha mizigo yake.
Alisema Tanzania imekuwa ikitumia ndege za Rwanda kusafirisha minofu ya samaki nje ya nchi wakati ikijipanga kununua za kwake ili kuongeza kasi ya biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Leave a comment