MGOMBEA urais wa Tanzania kupitia Chama cha Chaumma, Hashimu Rungwe, ametangaza kuzindua kampeni zake za urais wa chama hicho Jumamosi tarehe 5 Septemba 2020 Manzese jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Rungwe ambaye ni Mwenyekiti wa Chaumma amesema hayo leo Jumatatu tarehe 31 Agosti 2020 alipokuwa akizungumza na MwanaHALISI Online lililotaka kujua uzinduzi wa kampeni zake.
“Chaumma itaongea na wananchi 5 Septemba 2020 katika Uwanja wa Manzese Dar es Salaam kuanzia saa 8 mchana. Wananchi waje wasikilize, tunachowaambia. Wakija pale watapata kila kitu na watauliza maswali na tutawajibu,” amesema Rungwe
“Wako watu wenye hamu ya ubwabwa waje tutajua tunawapatiaje,” amesema
Rungwe ameahidi endapo akiingia madarakani baada ya uchaguzi mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020, atarejesha mfumo wa zamani wa kugawa chakula kwa wanafunzi shuleni.
Amesema, Serikali atakakayoiunda itahakikisha inagawa wali (ubwabwa) kwa wanafunzi shuleni ili kuwawezesha kusoma na kuwawezesha kufaulu vyema masomo yao.
Rungwe amesema, hakuna mtu asiyependa ubwabwa na Serikali yake itahakikisha hilo linafanyiwa kazi kwani mtu akishiba anaweza kufanya kazi.
Leave a comment