LOATA Ole Sanare, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro amewataka wazazi kufanyia kazi kwa vitendo maazimio mbalimbali yanayotolewa katika vikao vya kamati za shule ili kuinua ubora wa elimu shule za msingi na sekondari zilizopo. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Sanare ametoa kauli hiyo leo tarehe 2 Oktoba 2020 wakati alipotembelea kuona maendeleo ya Shule ya Msingi Juhudi iliyopo kata ya Lukobe, Manispaa ya Morogoro akisisitiza wazazi kujitolea kwenye ujenzi wa madarasa ya shule hiyo.
“Niwaombe wazazi, hawa ni watoto wetu na wanahitaji elimu bora, sasa kama sisi tunakwama, hata elimu bora watoto wataikosa” amesema Sanare.
Na kwamba, serikali inafanya kazi kubwa ya kuimarisha elimu kwa watoto, na wazazi pia wanayo majukumu ya kufanya kwa upande wao ikiwemo kuchangia katika ujenzi na michango ya chakula kwa watoto wawapo shuleni.
Amesema, ujenzi wa shule hiyo ulianza tangu Julai mwaka huu na kufanya shule hiyo kufunguliwa ikiwa na madarasa matatu mapya, mengine matatu yapo katika hatua ya upauaji.
Amesema, ujenzi wa shule hiyo ambayo ni Mkondo B wa Shule ya Msingi Lukobe kukamilika kwake kunategemea ushirikiano na nguvu za wananchi na serikali.
Sanare amesema, kama mkoa wanajipanga kutoa shilingi mil 20 kukamilisha ujenzi huo ambapo ujenzi huo utakapokamilia utakuwa umetumia kiasi cha shilingi mil 37.
“Imekuwa kama desturi sasa, mwaka jana watoto walinyimwa ripoti tukaambiwa twende na matofali mawilimawili ya block, tukapeleka ndipo tukapata ripoti sasa tena bado michango, mbona hatuelewi,” alisema.
Leave a comment