BARAZA la Taifa la Mitihani (Necta) nchini Tanzania, limetoa ratiba ya mitihani ya kidato cha sita na Ualimu mwaka 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ratiba hiyo imetolewa leo Ijumaa tarehe 22 Mei, 2020 na Necta ikionyesha mitihani ya kidato cha sita itaanza tarehe 29 Juni hadi tarehe 16 Julai, 2020.
Mitihani ya Ualimu nayo itaanza tarehe 29 Juni hadi tarehe 10 Julai 2020.
Akizungumza na MwanaHALISI ONLINE, Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Charles Msonde amesema, “kufuatia maelezo ya waziri (wa elimu) aliyoyatoa leo na Rais (John Magufuli) jana, tumeona tutoe ratiba ili wanafunzi waanze kujiandaa.”
Mapema leo asubuhi Ijumaa, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma aliitaka Necta kutoa ratiba mapema ya mitihani hiyo.
Wanafunzi hao walipaswa kufanya mitihani yao kuanzia tarehe 4 Mei, 2020 lakini iliahirishwa baada ya Serikali ya Tanzania kutangaza kuzifunga shule zote nchini humo kuanzia tarehe 17 Machi, 2020 ili kujikinga na maambukizi ya ugonjwa unaosababishwa na virusi vya corona (COVID-19).
Pia, vyuo vikuu na vya kati navyo vilifungwa kuanzia tarehe 18 Machi, 2020.
Hata hivyo, jana Alhamisi, Rais wa Tanzania, John Magufuli alitangaza kufunguliwa kwa vyuo vyote na wanafunzi wa kidato cha sita kuanzia tarehe 1 Juni, 2020.
Leave a comment