RAIS Mstaafu wa Awamu ya Pili, Alhaji Ali Hassan Mwinyi amesema anamhusudu Rais John Magufuli kutokana na mambo mazuri anayofanya kwa ajili ya maendeleo ya Tanzania bila kujali maslahi yake. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Dk. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 3 Oktoba 2018 ikulu jijini Dar es Salaam, ambapo ameweka wazi kuwa, utendaji kazi wa Rais Magufuli unagusa moyo wake na kwamba anatamani angekuwa kama yeye.
“Mtu anayefanya mambo mazuri ninamhusudu, na katika wanaokuhusudu kwa maana hiyo ni mimi mmoja wapo, kwa sababu unafanya mambo mazuri si kwa nafsi yako wala si kwa familia yako, bali mazuri kwa wananchi wa Tanzania, unaitakia Tanzania maendeleao ,kila jambo zuri unaipendelea Tanzania kuwa nayo, ningependa na mie niwe kama wewe,” amesema Alhaji Mwinyi.
Katika hatua nyingine, Dk. Mwinyi amesema anatamani kupata fursa ya kuwa karibu zaidi na Rais Magufuli kama baadhi ya watu wanavyodhani, ambapo baadhi yao wamekuwa wakimfikishia maombi yao kwa minajili ya kumtaka ayafikishe kwa Rais Magufuli.
“Kuna watu wanadhani niko karibu nawe sana kiasi kwamba shida zao waniambie mie ili mimi nikusogelee nikuambie hili kuna hili, fulani mfanyie hili, hayo si kweli natamani ingekuwa kweli, nataka usadiki mambo unayofanyia nchi hii yananigusa sana,” amesema.
Naye Rais Magufuli alimjibu akisema kuwa, anamhusudu kutokana na utofauti wake na kwamba anamuomba Mungu aendelee kumuweka ili Tanzania izidi kunufaika na uwepo wake.
“Mwinyi ulisema unanihusudu na mimi ninakuhusudu sana sababu ni rais uliye tofauti sana na Mungu amekujaalia unyeyekevu huo, ni suala la kumshukuru Mungu, tutanedelea kukuombea ili kusudi uendelee kuishi katika nchi hii ili na tunda hili tulilopatiwa na Mungu tuendelee kukutumia katika manufaa ya taifa,” amesema Rais Magufuli.
Leave a comment