RAIS wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi ametengua uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa Afya wa Wizara ya Afya, Dk. Jamala Adam Taib na Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja, Dk. Ali Salum Ali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Taarifa iliyotolewa leo jioni Jumatano tarehe 18 Novemba 2020 na Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dk. Abdulhamid Mzee imesema, viongozi hao watapangiwa kazi nyingine.
Dk. Mzee amesema, Rais Mwinyi amechukua uamuzi huo baada ya kufanya ziara Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja ili kujionea mwenyewe hali ya utoaji wa huduma na changamoto zinazoikabili hospitali hiyo.
Akiwa hospitalini hapo, Rais Mwinyi alitoa muda wa miezi mitatu kwa uongozi wa wizara ya afya kuhakikisha inarekebisha kasoro za kiutendaji zinazosababisha kutokuwepo ufanisi wa utoaji wa huduma bora.
Alisema kwa kiwango kikubwa mambo mengi yanahitaji kufanyiwa marekebisho, akibainisha kuwepo changamoto mbalimbali za kiutendaji na hivyo kuzorotesha uapatikanaji wa huduma bora kwa wagonjwa.
Rais Mwinyi alisema, analenga kuchukua hatua za kiutawala dhidi ya watendaji wasiowajibika kazini na kusababisha wananchi kulalamika kutokana na ukosefu wa huduma, pamoja na kupewa lugha zisizoridhisha kutoka kwa wauguzi na watendaji wengine wa hospitali hiyo.
Alisema pamoja na Serikali kuipatia fedha za kutosha hospitali hiyo kila mwezi, kumekuwepo changamoto za ukosefu wa vifaa muhimu kwa wagonjwa ikiwemo magodoro, dawa na vifaa vya maabara, hivyo akautaka uongozi wa hospitali hiyo kubadilika na kuondokana na utendaji wa mazowea.
Rais Mwinyi alisema, pale Serikali inapotoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa na hatimaye wagonjwa wakakosa dawa hizo, ni dhahiri kuna tatizo.
Alieleza kumekuwepo matatizo madogomadogo katika uendeshaji wa hospitali hiyo na kubainisha kama yangelishuhulikiwa ipasavyo ni wazi huduma bora zingepatikana.
Rais Mwinyi, aliahidi kufanya ziara nyingine siku zijazo na kuzungumza na wafanyakazi kwa lengo la kuimarisha utendaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
Alisema wafanyakazi wana wajibu wa kuwatumikia wagonjwa kikamilifu sambamba na kupata haki wanazostahili.
Leave a comment