RAIS John Magufuli amesema, kazi ya uongozi inahitaji uvumilivu pamoja na kumtanguliza Mungu katika kila jambo. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo tarehe 20 Oktoba 2019, Ikulu jijini Dar es Salaam katika hafla ya uapisho wa viongozi mbalimbali,aliowateua jana.
Akizungumza kwenye hafla hiyo, amesema wakati mwingine kazi ya uongozi ni kuchafuliwa badala ya kusemwa kwa mazuri.
“Saa nyingine katika uongozi inahitaji uvumilivu, kumtanguliza Mungu mbele. Utasemwa saa nyingine, usisemwe vizuri. Lakini hiyo ndiyo kazi ya uongozi. Kazi ya uongozi saa nyingine ni kuchafuliwa,” amesema Rais Magufuli.
Kauli hiyo ya Rais Magufuli imekuja katika kipindi ambacho kuna sintofahamu, kufuatia baadhi ya watu katika mitandao ya kijamii, kumzushia ugonjwa na hata wengine kudai kwamba ameaga dunia.
Kuhusu viongozi aliowaapisha, Rais Magufuli amewataka kuzingatia maadili, sheria na haki katika utekelezaji wa majukumu yao.
Miongoni mwa viongozi walioapishwa ni, Mathias Kabunduguru, aliyeteuliwa kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania.
Kabunduguru aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-TAMISEMI anayeshughulikia elimu, anachukua nafasi ya Hussein Katanga ambaye ameteuliwa kuwa Balozi.
Pia, Godfrey Mweli aliyeapishwa kuwa Naibu Katibu Mkuu TAMISEMI anayeshughulikia elimu. Awali, Mweli alikuwa Mkurugenzi wa Mipango wa Wizara ya Sheria na Katiba.
Kipngozi mwingine aliyeapishwa na Rais Magufuli ni Hashim Komba,Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea akichukua nafasi ya Rukia Muwango ambaye uteuzi wake umetenguliwa.
Hali kadhalika, Hassan Rungwa, ameapishwa kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea
Leave a comment