OFISI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ni chafu, hivyo Charles Kichere nenda kaisafishe. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kauli hiyo ameitoa Rais John Magufuli leo tarehe 4 Novemba 2019, wakati akimuapisha Kichere aliyemteua kuwa CAG, akichukua nafasi ya Prof. Mussa Assad.
“Ofisi ya CAG sio clean (safi) kama mnavyofikiria, nenda mkachague ili mauchafu uchafu haya ukayasafishe,” ameagiza Rais Magufuli na kuongeza;
“Nenda ukasimamie kazi yako vizuri. Na mwenzako aliyekuwepo amemaliza muda wake, kuanzia kesho unde ukafanye kazi. Nenda ukayatoe mauchafu uchafu hapo, mengine watakueleza wizara ya fedha.”
Rais Magufuli amemuagiza Kichere kuheshimu mihimili ya nchi, na kumtaarifu kwamba yeye ni mtumishi wa umma, hivyo asibishane na viongozi wa Bunge, Mahakama na Serikali.
“CAG mpya nakutakia kazi njema, usije ukaenda huko ukajifanya na we ni mhimili. Mihimili ni mitatu tu na umeiona hapa, kuna mahakama, bunge na serikali. Na katika kipato chako, nafasi yako ni mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali kwa hiyo mwenye serikali yupo,” amesema Rais Magufuli na kuongeza;
“Kafanye kazi zako vizuri za ukaguzi bila kuonea watu, unapopewa maagizo na mihimili mingine kama bunge katekeleze usijibishane nao. Ukipewa maagizo na mihimili mingine kama mahakama ukatekeleze wewe ni mtumishi lakini pia kasimamia ofisi.”
Wakati huo huo, Rais Magufuli amemtahadharisha Kichere kwamba, anaweza akaondolewa katika nafasi ya CAG kabla ya muda wake.
“Hapa mwanzoni Katiba inazungumza na sheria inazungumza, unaweza ukakaa miaka 5 au mwaka 1. Sababu taratibu za kukutoa zipo, na zinafanywa na rais. Lakini sikutishi nenda ukafanye kazi,” amesema Rais Magufuli.
Rais Magufuli amesema Kichere ana sifa pamoja na heshima, huku akieleza kwamba alipoondolewa katika nafasi mbalimbali, hakuzungumza, alikaa kimya.
“Najua una sifa nyingi tu, hukuwa kilaza kwa hiyo tunakuamini. Lakini pia, una heshima unatolewa ukamisha TRA hukutoa neno.
“Wapo wengine ukiwateua wanadhani ni nafasi zao. Ukimpa u-DC, ukimtoa analalamika, mbona hukulalamika wakati nakuteua?” amehoji Rais Magufuli.
Leave a comment