RAIS wa Tanzania, John Magufuli, amewawataka viongozi wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), wanaotarajiwa kuchaguliwa hivi karibuni, kuja na mipango madhubuti ya kukiimarisha chama hicho, pamoja na kuondoa kero za wanachama wake. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Rais Magufuli ametoa wito huo leo Ijumaa tarehe 5 Juni 2020 jijini Dodoma, wakati akizungumza katika mkutano mkuu wa uchaguzi wa chama hicho.
CWT inatarajia kufanya uchaguzi wa viongozi wake wapya, baada ya walioko madarakani kumaliza kipindi chao cha uongozi wa miaka mitano.
Akizungumzia uchaguzi huo, Rais Magufuli amewataka viongozi watakaochaguliwa, kutatua kero ya utitiri wa makato ya wanachama.
“Nafahamu uongozi utakaochaguliwa utaendelea kushughulikia makato ya asilimia mbili kwa kila mwanachama, suala ambalo wanachama hawakubaliano nalo wakidai ni kikubwa, lakini pia kiwango cha 200,000 kinachotolewa kwa mwanachama anapofariki hakitoshi ikilinganishwa na michango wanayotoa na hali ya maisha ya sasa,” amesema Rais Magufuli na kuongeza:
“Lakini pia wanachama wanapostaafu hupewa bati ishirini kama zawadi ambazo wanaona sio msaada kwao, na saa nyingine hazitolewi kabisa, haya ni baahdi ya mambo ambayo naamini mtakaochaguliwa pamoja na kwamba waliopo walianza kushughulikia, mkaendelee kushughulikia.”
Aidha, Rais Magufuli amewakumbusha viongozi watakaochaguliwa kwamba, jukumu lao ni kuwatumikia wanachama wao na si kutumia nafasi zao kujinufaisha.
“Na kwa wale viongozi watakaochaguliwa watambue wamechaguliwa kutumikia wanachama, kwa mujibu wa katiba za chama na kwamba dhamana waliyopewa ni utumishi na si njia ya kujipatia kipato,” amesema Rais Magufuli.
Rais Magufuli amewataka viongozi watakaochaguliwa kutumia rasilimali za CWT, kwa malengo yanayokusudiwa.
“Natoa rai kuchagua viongozi wazuri, hakikisheni uchaguzi uwe huru na ili muweze kupata viongozi waadilifu na wenye kujali masilahi yenu, chagueni viongozi wenye uchungu na lengo la kusaidia walimu, epukeni kuchaguana kwa kujuana au kutumia rushwa,” amesema Rais Magufuli.
Wakati huo huo, Rais Magufuli amejibu hoja ya CWT iliyotolewa na katibu mkuu wake, Deus Seif, kuhusu mafanikio na changamoto za chama hicho.
Seif ilimuomba Rais Magufuli kutatua changamoto ya uhaba wa walimu, nyumba za walimu, upandishaji wa madaraja na mishahara pamoja na malimbikizo ya madeni.
Akijibu hoja hiyo, Rais Magufuli amesema kuanzia Agosti 2018 hadi tarehe 3 Juni 2020, Serikali yake imelipa Sh. 1.2 trilioni, walimu wastaafu 15,029.
Amesema kuhusu walimu wastaafu 2,631 ambao wanadai Sh. 215 bilioni, watalipwa stahiki zao kabla ya mwezi Agosti mwaka huu.
Kuhusu changamoto ya uhaba wa walimu, Rais Magufuli amesema walimu wanaongoza kupewa ajira katika Serikali yake huku akisistiza kwamba, ataendelea kuwaajiri.
Leave a comment