RAIS John Magufuli ametuma salamu za pole kwa Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta kufuatia vifo vya watu 50 vilivyosababishwa na ajali ya basi la abiria linalomlikiwa na kampuni ya Western Express Sacco Limited, lililokuwa likitokea jijini Nairobi kuelekea Kisumu nchini humo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Rais Magufuli ametoa pole hizo katika ukurasa wake wa Twitter, kwa kuandika kuwa: “Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya ajali ya basi iliyotokea Kericho nchini Kenya na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 50. Nakupa pole Rais Uhuru Kenyatta, familia za marehemu na Wakenya wote. Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema na majeruhi wapone haraka. @UKenyatta.”
Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya ajali ya basi iliyotokea Kericho nchini Kenya na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 50. Nakupa pole Mhe. Rais Uhuru Kenyatta, familia za marehemu na Wakenya wote. Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema na majeruhi wapone haraka. @UKenyatta
— Dr John Magufuli (@MagufuliJP) October 10, 2018
Ajali hiyo imetokea leo Jumatano alfajiri ya tarehe 10 Oktoba 2018, katika barabara ya Londiani-Muhuroni, Kaunti ya Kericho nchini Kenya.
Ajali hiyo ilithibitishwa na Kamanda wa Polisi Kaunti ya Kericho, James Mogera ambapo alisema , miongoni mwa waliokutwa na mauti, ni watoto nane walio chini ya umri wa miaka mitano.
Kamanda Mogera alisema, majeruhi waliokuwa katika basi hilo lenye uwezo wa kubeba abiria 67, wamepelekwa katika Zahanati ya Fort Ternan na Hospitali ya Kaunti ya Muhoroni Sub kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
Chanzo cha ajali hiyo kinadaiwa kuwa basi kuvamia reli kisha kupanda katika shamba la mawe na kuanguka chini mita 20.
Leave a comment