RAIS wa Tanzania, John Magufuli amemteua Jaji wa Mahakama ya Rufani, Sivangilwa Sikalalilwa Mwangesi, kuwa Kamishna wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa ya uteuzi huo imetolewa leo tarehe 23 Desemba 2020 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais-Ikulu, Gerson Msigwa.
Taarifa ya Msigwa imesema Jaji Mwangesi ataapishwa kesho Alhamisi tarehe 24 Desemba mwaka huu, katika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma.
“Rais Magufuli amemteua Mheshimiwa Mwangesi kuwa Kamishna wa Maadili. Uteuzi wake unaanza leo tarehe 23 Desemba 2020 na ataapishwa kesho tarehe 24 Desemba 2020 saa 4:00 asubuhi, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma,” imesema taarifa ya Msigwa.
Jaji Mwangesi anachukua nafasi ya aliyekuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Mstaafu, Haroid Nsekela, aliyefariki dunia tarehe 6 Desemba mwaka huu.
Marehemu Jaji Nsekela aliteuliwa na Rais Magufuli kuwa Kamishna wa Maadili katika Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, mwezi Desemba 2016 na alihudumu katika nafasi hiyo hadi umauti ulipomkuta.
Leave a comment