RAIS wa Jamhuri, Dk. John Pombe Magufuli, amefanya mabadiliko madogo katika serikali yake. Ameteuwa waziri mmoja mpya; amehamisha mwingine na ameteuwa makatibu wakuu wapya. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu Kiongozi, John Kijazi, katika mabadiliko hayo, rais amembadilisha aliyekuwa waziri wa madini, Angellah Kairuki, kwenda kuwa waziri katika ofisi ya waziri mkuu (uwekezaji).
Naye Dotto Biteko, ambaye kabla ya mabadiliko hayo, alikuwa naibu waziri wa madini, sasa amefanywa kuwa waziri kamili katika wizara hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari, Ikulu jijini Dar es Salaam, leo tarehe 8 Januari 2019, Balozi Kijazi alisema, mabadiliko yaliyofanywa na rais yamelenga kuongeza msukumo kwenye masuala ya uwekezaji nchini.
Kabla ya mabadiliko hayo, hakukuwa na wizara ya uwekezaji, na kwamba wizara ya madini ilikuwa na manaibu waziri wawili. Lakini sasa, wizara hiyo, inakuwa na naibu waziri mmoja – Stanslaus Nyongo.
Kwa upande wa makatibu wakuu, rais amemhamisha aliyekuwa katibu mkuu (Ujenzi), Joseph Nyamuhanga, kwenda kuwa katibu mkuu, ofisi ya rais (Tamisemi).
Wengine, ni Zainabu Chaula aliyefanywa kuwa katibu mkuu (afya) kutokea Tamisemi; Elius Mwakalinga, alifanywa kuwa katibu mkuu (ujenzi) na Dorothy Mwaluko aliyefanywa kuwa katibu mkuu, ofisi ya waziri mkuu (uwekezaji).
Dk. Dorothy Gwajima ambaye amefanywa naibu katibu mkuu (Tamisemi) na Dk. Francis Michael, amefanywa kuwa naibu katibu mkuu utumishi.
Aliyekuwa katibu mkuu, wizara ya afya, Dk. Mpoki Ulisubisya, amefanywa kuwa balozi. Kituo chake cha kazi kitatangazwa baadae.
Serikali imefungua pia ubalozi nchini Cuba; balozi wake atateuliwa siku za usoni.
Balozi Kijazi amesema, mabadiliko yamefanyika ili kujaza nafasi za baadhi ya waliostaafu na kuimarisha, “utendaji katika wizara mbalimbali.”
Leave a comment