RAIS John Magufuli ameweka msisitizo kuwa, serikali haitatoa msaada wa aina yoyote kwa watu waliojenga mabondeni, pindi watakapopata maafa ya mafuriko. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza na wakazi wa Kigamboni jijini Dar es Salaam, leo tarehe 11 Februari 2020, Rais Magufuli amesema, serikali haitahangaika kusaidia mtu atakayekumbwa mafuriko mabondeni, sababu wameyataka wenyewe.
“Hakuna cha kusaidiwa, uliyatafuta mwenyewe hayo mabonde ngoja yakubondoe ili ujifunze mwenyewe. Nataka kuwaeleza ukweli ndugu zangu sitaki unafiki,” amesisitiza Rais Magufuli.
Rais Magufuli amewalaumu watu waliojenga makazi yao mabondeni na kuacha kujenga sehemu zenye miinuko, huku wakijua dhahiri kwamba maeneo hayo huwa yanakumbwa na mafuriko ya mara kwa mara kwa kuwa ni mkondo wa maji.
“Mlima upo hutaki kujenga kwenye milima unajenga kwenye bonde, nilimtuma waziri mkuu na ameshatoa maelekezo kwamba wale waliojenga mabondeni ambako wana uwezekano wa kupata maji, wahame wenyewe,” amesema Rais Magufuli na kuongeza:
“Na wala serikali haitahangaika na mtu aliyejipeleka kwenye bonde mwenyewe halafu ishughulikie kumlisha, Uwe uko Chato, uwe wapi huo ndio msimamo, acheni kujenga kwenye mabonde.”
Wakati huo huo, Rais Magufuli amewataka Watanzania kutumia vyema mvua, kwa kufanya shughuli za kilimo.
“Kila Mtanzania mahali alipo afanye kazi, walime mazao yanayostahili hata ukame mvua ikinyesha wewe kalime viazi, wakiwa wanafurika huko wewe unalima miogo, kunde.
Wakiwa wanafurikwa huko wewe unafanya kazi ili baadae wanapotoka kwenye mafuriko waje wale chakula chako kwa kuwatwanga pesa hayo lazima niwaleleze,” amesema Rais Magufuli.
Leave a comment