WAZIRI wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo ameiagiza bodi mpya ya wakurugenzi wa Wakala wa Nishati ya Umeme Vijijini (REA) kuwakagua wakandarasi wote ambao wamepata tenda ya usambazaji wa umeme vijijini, anaandika Dany Tibason.
Mbali na kutoa agizo la kuwakagua wakandarasi pia REA wametakiwa kuhakikisha wanatumia vifaa vinavyozalishwa ndani ambavyo vina ubora badala ya kuagiza vifaa vya umeme kutoka nje ya nchi.
Akizungumza na wajumbe wapya wa Bodi mpya REA, Prof. Muhongo amesema bodi hiyo inatakiwa kuwa na malengo mapana kwa ajili ya kuhakikisha umeme unawafikia wananchi kwa kiwango kikubwa.
Prof. Muhongo amewataka wajumbe hao wa bodi kuhakikisha wanapokea makablasha kabla ya wiki mbili ili waweze kuyapitia mapema na kuyasoma.
Katika kuhakikisha umeme unakuwa kichocheo cha maendeleo ni vyema umeme huo ukawekewa katika taasisi mbalimbali ili kuwapatia umeme.
“Sasa katika kutekeleza umeme unakuwa kichocheo, ni vyema umeme usivuke taasisi mbalimbali kama vile, shule zote za sekondari na shule za msingi, zahanati hospitali, mashamba makubwa na katika sehemu za kibiashara,” amesema.
Katika uzinduzi huo Prof. Muhongo, ameitaka bodi hiyo kuhakikisha inasimamia zaidi ubora wa vifaa vya umeme ambavyo vina ubora.
“Nawaagiza nyie bodi kuhakikisha mnaponunua vifaa vya umeme kuhakikisha vinakuwa na ubora na vinavyozalishwa,” amesema Prof. Muhongo.
Aidha amesema makampuni yote ya kutoka nje ya nchi ambayo yanafanya kazi ndani ni lazima kuwa na wakandarasi wadogo wa ndani na si vinginevyo.
“Haiwezekani kwa mfano nguzo za umeme zinapatikana hapa Iringa, lakini unaweza kushanga eti nguzo zinaagizwa kutoka Afrika Kusini na maeneo mengine,” amesema.
Leave a comment