DIANA Simba, mwanachama wa Chama cha Wananchi (CUF) leo tarehe 13 Machi 2019, amejitokeza na kumwaga sera kwamba, anaweza kuongoza chama hicho bila shaka yoyote. Anaripoti Regina Mkonde…(endele).
Ni nafasi ambayo Prof. Ibrahimu Lipumba pia anainyemeleza baada ya kumaliza kipindi chake cha miaka mitano ya uongozi wake ndani ya chama hicho kilicho na mgogoro wa kiutawala kwa miaka mine sasa.
CUF ipo kwenye mchakato wa kuwapata viongozi mbalimbali ikiwa ni pamoja na nafasi ya mwenyekiti wa chama hicho licha ya kuwepo kwa mgogoro mzito uliokigawa chama hicho vipande viwili.
Makundi mawili yameibuka ndani ya chama hicho moja likumuunga mkono Prof. Lipumba, mwenyekiti wa chama hicho anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ambapo kundi la pili linaungwa mkono na Maalim Seif Shariff Hamad, Katibu mkuu wa chama hicho.
Kwenye mkutano mkuu ulioanza jana tarehe 12 Machi 2019, mgombea Diana amesema, naye ni msomi kama Prof. Lipumba kwani ana Stashahada ya Maendeleo ya Jamii.
Diana ndiyo mwanamke pekee anajitokeza kugombea nafasi ambapo alikutana na wakati mgumu kutokana na baadhi ya wajumbe wa chama hicho hususan wanawake kumbeza.
“Nilijiunga na chama mwaka 2017 na nimetembelea Kenya na Uganda, msifikiri Profesa Lipumba ndiye msomi peke yake, hata mimi ni msomi. Nina Diploma ya Maendeleo ya Jamii hivyo nina uwezo wa kuwaongoza,” amesema Diana.
Kwenye mkutano huo wagombea wengine ni Prof. Lipumba na Zuberi Hamisi.
Uchaguzi huo unafanyika ili kujaza nafasi baada ya Prof. Lipumba kumaliza muda wake ikiwa ni pamoja na muda wa uchaguzi kufika kwa mujibu wa katiba ya chama hicho.
Wajumbe hao waliohudhuria mkutano wa saba wa CUF ulioanza jana na ambao unatarajiwa tarehe 13 Machi 2019 katika ukumbi wa Hoteli wa Lekam ulioko Buguruni jijini Dar es Salaam.
Prof. Lipumba pamoja na wagombea wengine, walinadi sera zao mbele ya wajumbe wa mkutano huo, wakiwataka kuwachagua ili washikilie cheo hicho.
Prof. Lipumba anapewa kipaumbele na wajumbe hao katika kuchaguliwa kukishikilia kijiti hicho kwa mara nyingine tena, kutokana na uzoefu wake kuhusu masuala ya siasa za ndani na nje ya CUF.
Katika uchaguzi huo, wajumbe hao wa CUF kambi ya Prof. Lipumba wanatarajia kuchagua makamu mwenyekiti wa CUF kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara.
Leave a comment