Friday , 29 March 2024
Home Gazeti Makala & Uchambuzi Prof. Lipumba ageukwa na Swahiba wake, Abas Mhunzi
Makala & Uchambuzi

Prof. Lipumba ageukwa na Swahiba wake, Abas Mhunzi

Prof. Ibrahim Lipumba
Spread the love

ABAS Juma Mhunzi, makamu mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Tanzania Zanzibar, “ameliamsha dude.” Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).

Amemtuhumu mwenyekiti wake, Prof. Ibrahim Lipumba, kuendesha chama chao kama kampuni binafsi.

Katika andishi lake alilolisambaza kupitia  makundi sogozi (WhatsApp), Mhunzi anasema, “nafahamu kuwa CUF kinaendeshwa kimakundi, lakini sikuwa nafahamu kwamba huo ndio uendeshaji wa chama kiprofesa.”

Anasema, “siku zote natukanwa na kushambuliwa katika Baraza (Baraza Kuu la Uongozi la taifa la CUF), huku nikishangaa kwa nini mwenyekiti (Prof. Lipumba), haingilii hoja za kusambaratisha chama kama zinavyotolewa na kundi linalotambuliwa rasmi na viongozi wakuu wa chama.”

Anasema, sababu ya yeye kushambuliwa na Prof. Lipumba kunyamazia vitendo hivyo, ni “eti kumshauri mwenyekiti vibaya kuteuwa wakurugenzi.”

Anasema, lakini kama hoja ni kundi maarufu la G9, kwamba wanahisi kuwa hadi leo yeye ndiye aliyewatenga, basi kuna siku ukweli utajulikana.

Mhunzi ambaye alikuwa mjumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BWW), kwa takribani miaka 15 anasema, alidumu katika nafasi hiyo kutokana na kuwa muwazi mpaka akafungiwa mwaka mmoa kushiriki mikutano ya baraza la wawakilishi.

“Nilifungiwa mwaka mmoja bila kulipwa mshahara. Nikaenda mahakamani na kushinda. Baadaye nikapewa jina na Wazanzibari, kwa kuitwa, “Msema Kweli.”

Ndani ya baraza la wawakilishi, Mhunzi alikuwa mwenyekiti wa Kamati ya Kuchunguza Mahesabu ya Fedha na Uchumi ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (PAC).

Wakati huo, alikuwa mwakilishi wa jimbo la Chambani kupitia chama hicho.

Abas Juma Mhunzi, makamu mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Tanzania Zanzibar (aliyesimama)

Katika andishi lake hilo kuhusu CUF, Mhunzi anasema, viongozi wenzake hawampi taarifa yoyote kuhusiana na chama kinavyokwenda na hata pale anaposhauri hubezwa.

Andishi la Mhunzi limepatika siku moja baada ya kusimamishwa wadhifa wake wa makamu mwenyekiti. Wapo wanaosema, hata kufukuzwa kwake, kumetokana na usambazaji wa andishi hilo.

Anasema, “yawezekana ninayouliza yanakera. Nauliza kuhusu fedha Sh. 1.115 bilioni, zilizotokana na malimbikizi ya ruzuku ya chama kutoka kwa Msajili wa Vyama vya Siasa, kwamba zimetumikaje? Nauliza haya kwa kuwa hata Zanzibar hatujapewa tukaimarisha chama kilichoathiriwa vibaya na mgogoro.

“Nilishauri sana kuwa Katiba lazima ifuatwe na katibu mkuu ambayo ni nafasi ya Zanzibar, lazima aje Zanzibar tusaidiane kufufua chama. Mkubwa hakutaka.

“Nimeshauri Zanzibar nasi tupatiwe gari tatu ili zisaidie kazi ya kuimarisha chama. Badala yake, tukamegewa Sh. 15 milioni pekee kwa Zanzibar nzima, yaani Unguja na Pemba. Kwamba, eti tutumie gari moja. Labda viongozi hawafahamu kuwa Unguja iko kilomita za bahari 70 kutoka Pemba.

“Nilishauri na sisi Zanzibar tufanyiwe semina ya viongozi kama iliyofanywa Bara, lakini wakubwa hawakukubali. Mimi kosa langu nini wenzangu? Kwa sababu tu naitetea Zanzibar kichama na mimi naitwa Makamo wa Zanzibar.

“Katika fedha zinazoletwa Zanzibar ni Sh. 5 milioni pekee, ndio za kufanyia siasa na hizi hatuwezi kufanya jambo kubwa kwa kuwa kuna matumizi ya lazima sana ambayo hatukuweza. Hatukuwa na ofisi Pemba ambako iko ngome ya upinzani na tumelazimika kukodi ofisi ya kuwakusanya angalau viongozi wa Pemba. Kosa langu liwapi?

“Tumelazimika kulipia kodi nyumba ya Naibu Katibu kwani Bara hawaleti fedha. Nasikia baadhi ya wakurugenzi Bara wanalipiwa pango na iliahidiwa ndani ya Baraza Kuu, kwamba ikifika mwezi huu (Mei), zingelipwa na kwa kweli, zimelipwa kwa Bara. Lakini Zanzibar hapana kitu na hata Wakurugenzi wangu wakiuliza wanabezwa.

“Nimesema sio sahihi kwa Kamati ya Mashauriano Bara kuendesha chama kwa remote bila kuzingatia Katiba. Hakuna anayejali.

“Kamati ya mashauriano inatoa Kanuni za uchaguzi na hii ni kazi ya Baraza Kuu, mimi nikihoji, naitwa kiherehere; mkurugenzi wa mipango ndiye bingwa wa kuichambua Katiba niliyoshiriki kuitunga.

“Katika namna makundi yanavyopewa nguvu hata kwa Bara, kiongozi sasa anafikia hatua ya kumdunda mjumbe ndani ya Kamati Tendaji, lakini Naibu Mkurugenzi wa Itifaki yupo kikaoni na hachukuwi hatua.

“Hii ni kwa sababu ni miongoni mwa vipenzi vya mwenyekiti. Aweza kufanya lolote kwa kuwa ana haki kuliko wengine. Hii si Haki wala si Furaha ndani ya chama.

“Mwenyekiti anahakikisha kuwa haitishi kikao pamoja mimi na Maftaha (Mataha Namchuma, makamu mwenyekiti Bara), kwa sababu tutamshauri asiyoyataka.

“Nimeshauri kuwa kwa vile kuna Corona isiwe sababu kuvunjwa Katiba. Kamati ya uongozi na almost Kamati ya Itifaki ndizo zenye sura ya kimuungano zikutane ku control chama kuelekea uchaguzi.  Mwenyekiti hataki, tena nasema hataki.

“Nimemshauri sasa ni wakati zaidi ya siku 50 tokea katibu mkuu (Khalifa Suleman Khalifa), afariki dunia tukutane angalau tuyazungumze; hajibu. Mwaka mmoja uliopita nimefanya kazi za katibu mkuu hadi leo tunaingia katika uchaguzi hataki hata kutuona pamoja na kwamba tumempigia hadi simu.

“Lakini ilipoombwa na Musa Haji Kombo kutolewa fedha ili akapachike bendera Pemba, kwa kuwa eti sisi ni woga, alipewa na hakuna bendera iliyopachikwa, lakini mwenyekiti aliona sawa kwa kuwa Musa wanasafiri dau moja.

“Tumepewa ofisi za makao makuu zikiwa hazina hata vyoo kutokana na kuvunjwa na tumelazimika kununua na vitendekazi na fanicha kwa pesa hiyo hiyo aliyotaka kilaghai 5 milioni. Tutapata wapi pesa ya kufanyia siasa.

“Leo badala ya kutupa fedha tutumie kwa kuimarisha chama, eti kilaghai, anatuma milingoti na kwa kuwa hatukupachika milingoti kwa kuheshimu  Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na huu ni uamuzi wa kikao, leo kinatumwa kikosi kazi kabla hatujamaliza kufunga ili kuwaonyesha wajumbe kuwa wao ni bora kuliko sisi tukaao ofisini kula fedha.

“Hivi ndivyo uongozi unavyoshiriki kukigawa chama. Wajumbe wa Baraza wa Zanzibar waliniamrisha niwaitishe kikao na nikakubali. Agenda yao siku ile ilikuwa wanataka Katibu mkuu achaguliwe miongoni mwao. Nikawauliza mnaye mtu wa kushika nafasi hiyo? Wakasema, ‘ndio.’”

“Mimi si Profesa lakini  ni meneja na mtawala wa kusomea na kupractice. Nikawawahi kwa kuwaambia musimtaje. Nilikuwa nyimbo ya kufunzwa haikeshi.

“Siku ya pili alikuja Mbwana ofisini kwangu na kunipongeza nilipowazuia wasimtaje mtu wanayetaka kupewa nafasi ya katibu mkuu.

“Nikamuuliza kwa nini? Akanambia usiku kazungumza na mwenyekiti na kamtajia watu anaowataka. Akanitajia. Nikasema, sawa. Kama mwenyekiti anaweza kuzungumza na Mbwana kwa wasaa lakini anashindwa kushauriana na mimi msaidizi wake. Hii ni ajabu.

“Hakuna sababu kwa nini Zanzibar haina Katibu mkuu isipokuwa mwenyekiti hataki. Nafahamu kwa nini na iko siku nitaomba radhi Wazanzibari niseme kilicho nyuma ya pazia. Mwenyekiti alinipigia simu kuwa Abdul Kambaya kaomba ajiuzulu kwa hivyo nakupa haribu unishauri.

“Nikamwambia muliloamua na Maftaha kwa Bara ni sawa. Na mimi baada ya Mwezi mmoja nikamwambia kanijia Mkurugenzi wa Zanzibar anataka kuandika barua ya kujiuzulu, lakini nimemsihi asiandike barua.

Leo mwenyekiti nakushauri umbadishe na hata ikiwezekana morning nafasi G9. Leo anawaita G9 nyumbani kwake anawatia fitna wanipinge mimi kwa sababu nikifungua mdomo naitaja Zanzibar ambayo hataki kuisikia.

“Zanzibar tunaingia mwaka wa pili tukiwa na wajumbe pungufu wa kikatiba na nimemwandikia Mkubwa wangu hataki. Haya niliyoyataja hapa ni ya kawaida sana na makubwa zaidi yatamfedhehesha mkubwa wangu, lakini namuomba aitishe Baraza Kuu ili wanihukumu na wanao uwezo huu.

“Mimi sipapii uongozi, tofauti na wengine waliotayari hata kuuwa. Mimi naringia  wanachama wangu na kuona CUF haifi pamoja na kutaka kuuliwa na aliekiunda.

“Hivi kweli Masoud wa Tanga na Othmani wa Micheweni watakuwa na uwezo wa kuifufua CUF mkoani na Chakechake kuliko mimi niliecheza na siasa miaka 30!

Huu ni usanii wa Mwisho au yawezekana kwa kuwa sikuwa mwana mikakati ya kumuomdosha ndio malipo yangu haya. Yawezekana mwenyekiti wa taifa akampigia simu Blue Guard amnunulie madira ya kuimarishia chama Pemba. Yawezekana mimi nikaenda Pemba kuonana na wajumbe wa tukakubaliana.

Fatua halafu MBWANA amshitakie Mwenyekiti azungumze na Afisa Dawati abadilishe maamuzi yetu. Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Chake walimsimamisha Baha kwa kutumia 1?200,000 za wilaya mimi nikasema, Katiba inaruhusu leo Ali Jabir na Mbwana wanamchukua BAHA ndani ya vikao vya Kamati Tendaji na kumwambia ilivyokuwa hajapewa barua yeye BAHA ndie Katibu wa wilaya na Mbwana ndie mshauri wa Mwenyekiti wa Pemba.

“Mbona Masoud wa Wete Jawa Katibu wa Wilaya badala ya Sharrif ambae hata sisi hatuna taarifa kama Viongozi wa Zanzibar. Namalizia kwa kusema kuwa ingekuwa si fitna kubwa anazojengewa mwenyekiti na yeye kuzikubali na akakubali usanii wa Masudi na wenziwe wachache wa Kamati Tendaji ambao nawafahamu sasa CUF ingekuwa mbali sana.

“Nimesikia michango ya baadhi ya wajumbe wakisema Maalim Seif aliwanyanyasa sana Wabara na leo Wanaugeuza wembe. Walichokuwa hawakifahamu ni kimoja tu. Katika wanaonyolewa wamo wendawazimu.

“Yameenezwa uongo kuwa sisi viongozi wa Zanzibar kazi yetu ni kukaa ofisini tukila pesa tu. Nawaomba Wajumbe wa Baraza Kuu waunde kamati ya uchunguzi sio tu kwa Zanzibar, lakini kwa chama chote ili tuwafahamu wanaoiba fedha ya chama.

“Kidogo nilichokiona juzi tu ni Kanuni za Uchaguzi picha kwamba Kamati Tendaji haina mamlaka ya kuzisambaza, lakini watwambie idhini ya matumizi ya FEDHA? yakuchapisha Kaninu zilizotumwa wilayani bila hata ya uongozi Zanzibar hata kuarifiwa.

“Naomba Lipumba itisha kikao unifukuze au tupange namna ya kuingia katika uchaguzi. Chama hakiendeshi sawa nachukia sana na mimi kuandika hapa ni kuvunja utamaduni wa uongozi niko tayari kuwajibika ili G9 waendeshe chama Lipumba anavyopenda.” 

Mhunzi amepata kuwa maarufu mkubwa wakati alipokuwa mwakilishi wa Chambani, kutokana na msimamo wake wa kupinga matumizi mabaya ya fedha za umma.

Aliwahi kukumbana na matatizo kadhaa, ikiwamo kufikishana mahakamani na aliyekuwa Spika wa Baraza la Wawakilishi, Pandu Ameir Kificho, baada ya kupewa adhabu ya kutohudhuria katika vikao kwa mwaka mzima.

Adhabu hiyo ilitolewa baada ya Mhunzi kukataa kuomba radhi barazani kufuatia kauli yake kuwa bei za mafuta zinapangwa Ikulu.

Katika kadhia hiyo, Spika Kificho alimuamuru Mhunzi kutohudhuria vikao kwa mwaka mzima, lakini mwakilishi huyo alipinga mahakamani na kushinda kesi na kulipwa haki zake.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Miaka 28 watumishi UDSM yaliwa na nzige, madumadu

Spread the loveGEORGE Francis anasikitika; anatembea akiwa na mawazo mengi, hajui la...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nimekumbuka Samia wa miaka 3 iliyopita

Spread the loveWAKATI naandaa makala ya safu hii wiki hii, nimejikuta nakumbuka...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Hakuna fedha za Rais

Spread the loveKUNA mambo machache mazuri ya kujifunza kutoka kwa Margaret Thatcher,...

error: Content is protected !!