PROFESA Palamagamba Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, amekanusha kauli inayosambaa katika mitandao ya kijamii ya kwamba amethibitisha kuwa mwanahabari Azory Gwanda amefariki dunia. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Dk. Hassan Abass, Msemaji Mkuu wa Serikali katika ukurasa wake wa Twitter, imemnukuu Prof. Kabudi akisema kwamba, mpaka sasa hakuna uthibitisho kuwa Azory yuko hai au amefariki.
Prof. Kabudi amesema amepokea kwa masikitiko tafsiri zilizotolewa na baadhi ya watu, kufuatia kauli yake aliyoitoa wakati akihojiwa kwenye kipindi cha BBC Focus on Africa, kwa kuwa tafsiri hizo zimemnukuu kimakosa.
“Nimepokea kwa masikitiko taarifa potofu zinazoendelea kuchapishwa kwenye mitandao ya kijamii ikinukuu kimakosa mahojiano yangu kwenye kipindi cha BBC FOCUS ON AFRICA zikidai kuwa nimethibitisha kwamba mwanahabari Azory Gwanda amefariki dunia,” amefafanua Prof. Kabudi na kuongeza.
“Mpaka sasa hakuna uthibitisho kuwa Azory yuko hai au amefariki. Vyombo vya ulinzi na usalama vinaendelea kuchunguza tukio hilo na matukio mengine yaliyotokea katika machafuko ya Kibiti, Pwani yaliyosababisha ama watu kadhaa kupoteza maisha au kupotea.”
Prof. Kabudi amesema katika mahojiano hayo alieleza kwamba tukio hilo lililotokea Kibiti mkoani Pwani ni la kuhuzunisha na wapo Watanzania waliouwawa na wengine kupotea.
“Hii sio tafsiri sahihi kuhusu kile nilichokisema. Katika mahojiano hayo nilieleza kuwa tukio lililotokea Kibiti lilikuwa ni la kuhuzunisha na wapo watanzania waliouwawa na wengine kupotea. Sikuthibitisha kuwa Azory Gwanda amefariki.”
Leave a comment