KIWANGO cha posho wanacholipwa Wenyeviti wa Serikali za Mitaa nchini, kimezua mjadala bungeni. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mjadala huo ulianza baada ya Hassani Kaunje, Mbunge wa Lindi Mjini, kuhoji lini serikali itaanza kuwalipa posho au mishahara wenyeviti wa serikali za mitaa.
Kufuatia swali hilo, wabunge kadhaa waliibuka na kuhoji, lini serikali itaongeza kiwango cha posho kwa wenyeviti hao, pamoja na kuwadhamini ili waweze kupata mikopo kama inavyofanya kwa madiwani na wabunge.
Akijibu maswali hayo, Mwita Waitara, Naibu Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, amesema sheria inaelekeza kwamba, wenyeviti watalipwa posho na halmashauri husika, kulingana na mapato yanayokusanywa na halmashauri zao.
Waitara amesema, Wenyeviti wa Serikali za Mitaa wanashindwa kupata mikopo, kwa sababu ya kutokuwa na kipato cha uhakika, kutokana na kulipwa kiwango kidogo cha posho, hasa kwa halmashauri zisizokuwa na mapato ya kutosha.
“Ni kweli wenyeviti wanafanya kazi kubwa na serikali inawathamini, mapato wanayopewa ni kutokana na uwezo wa makusanyo ya halmashauri, kadri wanavyobuni miradi wenyeviti wao watapata posho. Lini wenyeviti wataanza kupata mkopo, ni kweli hiki kiwango ni kidogo, kukopesheka benki inakuwa ngumu,” amejibu Waitara.
Baada ya majibu hayo, Job Ndugai, Spika wa Bunge ameshauri Wizara ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI, kutoa muongozo wa kiwango cha posho, watakacholipwa wenyeviti wa serikali za mitaa nchi nzima.
Ndugai amesema kitendo cha wenyeviti wa serikali z amitaa kulipwa kiwnago tofauti cha posho, kinaleta mkanganyiko miongoni mwao, kutokana na baadhi yao kulipwa posho ndogo.
“Hili swala la posho za madiwani na wenyeviti, ningependa kuwashauri TAMISEMI lina matatizo makubwa sana. Ambalo ufumbuzi wake ni TAMISEMI, hii lugha kusema halmashauri ilipe kutokana na uwezo wake hili ni tatizo kubwa, “ amesema Ndugai na kuongeza;
“Kwa nini isiwekwe muongozo nchi nzima wenyeviti wanalipwa hivi. Watu wanavunjika moyo, kwa nini malipo yasijulikane tu, kama kongwa laki , naomba tamisemi muliangalie hili. Toeni muongozo malipo ni haya.”
Leave a comment