BAADA ya Jeshi la Polisi kumuhoji Kiongozi wa Chama cha Act-Wazalendo Zitto Kabwe jeshi hilo linatarajia kuihoji Kamati nzima ya Uongozi wa Chama hiko, anaandika Hamis Mguta.
Mapema Tarehe 31 Oktoba Zitto kabwe alitiwa mbaroni akiwa nyumbani kwake na kupelekwa kituo cha Polisi cha Chang’ombe wilayani Temeke, Dar es Salaam baadaye kuachiwa kwa dhamana kisha kukamatwa tena kwa amri ya Mkuu wa Upelelezi wa Polisi (DCI) na kuhojiwa kwenye kituo cha Makosa ya fedha na uchumi kilichopo Kamata Kariakoo na kuachiwa tena kwa dhamana.
Kaimu Mwenyekiti wa Chama hiko Yeremia Maganja leo juma pili amesema kuwa Tarehe 2 Novemba chama hiko kimepokea wito (summons) kutoka Jeshi la polisi wa kuhojiwa kwa kamati kuu ya chama na wanatakiwa kufika kwenye kituo hiko cha makosa ya Fedha Tarehe 6 Novemba mwaka huu.
Maganja ameeleza kuwa ameshangazwa na jeshi hilo kuingilia huru wa vyama vya siasa na kwamba kamati ya chama hiko ipo kihalali na kikatiba.
“Tangu tuzindue kampeni zetu katika kata ya kijichi, Jeshi la Polisi limefanya maamuzi ya kushikilia au kuhitaji kuhoji viongozi wetu, maamuzi ambayo yanaathiri kampeni zetu,” amesema.
Amesema kuwa uwamuzi wa chama ni kuendelea na kampeni kama kawaida, hivyo polisi watafute namna ya kufanya mahojiano na viongozi wa chama hiko.
Leave a comment