WAKATI kesi Na. 112/2018 ya uchochezi inayowakabili Freeman Mbowe na viongozi wenzake wa Chadema, Jeshi la Polisi limeendesha zoezi la kuwasomba wafuasi wa chama hicho katika viunga vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu. Aripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Polisi waliendesha zoezi hilo muda mchache baada ya kutoa tangazo kwa wafuasi wa chama hicho, waliojitokeza kusikiliza hukumu hiyo leo tarehe 10 Machi 2020.
Mbowe na wenzake wanakabiliwa na mashtaka 13 ikiwemo kula njama, kufanya mkusanyiko usio halali.
Wengine wanaokabiliwa na kesi hiyo ni Dk. Vicent Mashinji, aliyekuwa katibu mkuu wa chama hicho; John Mnyika, Katibu Mkuu wa chama hicho, Salum Mwalimu; Naibu Katibu Mkuu (Zanzibar).
Yumo Peter Msigwa; Mbunge wa Iringa Mjini; Esther Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini; Halima Mdee, Mbunge wa Kawe; Ester Bulaya, Mbunge wa Bunda na John Heche, Mbuge wa Tarime Vijijini.
Wafuasi hao ambao awali walitaka kuingia wote kwenye chumba cha mahakama, walizuiliwa na kubaki katika viunga vya mahakama hiyo, ambapo waliambiwa watulie sambamba na kukaa chini.
Hata hivyo, utulivu ulioelezwa na polisi haukuwepo na ndipo polisi waliamua kuwatoa nje ya viwanja vya mahakama. Kutokana na kuondolewa kwenye viwanja vya mahkama, walianza kuimba nyimbo za kuwatuhumu polisi.
Hali hiyo ilisababisha polisi kuanza kukamata wafuasi hao na kuwaingiza kwenye gari la polisi (defender) na kisha kutokomea nao. Mpaka sasa, idadi ya wafuasi wa Chadema waliokamatwa na polisi, haijajulikana.
Leave a comment