ASKARI watatu wameripotiwa kufariki katika ajali ya gari ya Polisi mkoa wa kipolisi Rufiji iliyotokea baada ya gurudumu la nyuma la gari hiyo kupasuka na kusababisha gari kupinduka. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
SACP David Misime, Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini leo amewaambia waandishi wa habari kuwa ajali hiyo imetokea jana tarehe 25 Julai 2019 majira ya saa saba mchana katika kijiji cha Kilimahewa wilayani Mkuranga, Rufiji.
Gari hilo Toyota Land Cruiser lenye namba za usajili PT. 3822 lilikuwa likitokea Ikwiriri kuelekea Kijiji cha Mwalusembe, lilipasuka gurudumu moja la nyumba upande wa kulia na kusababisha kupinduka.
“Askari waliofariki kwenye ajali hiyo ni aliyekuwa Afisa Mnadhimu Rufiji, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Issah Bukuku na Inspekta Esteria wa Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Kipolisi Rufiji pamoja na namba G.1132 PC Lameck wa Kikosi cha kutuliza ghasia (FFU) mkoani humo,” amesema.
Waliojeruhiwa ni F.7167 PC Ibrahim ambaye ndio alikuwa dereva wa gari hilo pamoja na F.7651 PC Mgusi wa ofisi ya Kamanda wa Polisi Rufiji.
SACP Misime amesema kuwa majeruhi wote wawili wamefikishwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu.
Leave a comment