JESHI la Polisi Mkoa wa Kinondoni, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, imefanya upekuzi nyumbani kwa Msanii, Idris Sultani, maeneo ya Mbezi Beach jijini Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Idris ambaye ni msanii wa vichekesho nchini Tanzania, anashikiliwa katika Kituo cha Polisi cha Oysterbay tangu tarehe 19 Mei, 2020, akituhumiwa kwa makosa ya mtandaoni.
Akizungumza na Mwanahalisi Online kwa simu leo Alhamisi tarehe 21 Mei, 2020, Benedict Ishabakaki ambaye ni Wakili wa Idris, amesema msanii huyo amepekuliwa nyumbani kwake kwake jana Jumatano jioni, alirudishwa tena katika Kituo cha Oysterbay.
“Jana walienda kupekua nyumbani kwake majira ya jioni, tulivyorudi kituo cha Oysterbay tukawa tumeshindwa kutimzia masharti ya dhamana kwa sababu ilikuwa usiku.”
“Lakini dhamana yake iko wazi, kwa hiyo sasa hivi tuna shughulikia dhamana yake polisi,” amesema Wakili Ishabakaki.
Wakili Ishabakaki amesema, polisi kituoni hapo wanatarajia kumhoji Idris wakati wowote kuanzia sasa.
Pia, amesema polisi kituoni hapo wamesema dhamana ya mchekeshaji huyo iko wazi, na kwamba anatarajia kutoka akishamaliza mahojiano pamoja na kutimiza masharti ya dhamana.
“Lakini leo ataanza mahojiano maana alikuwa bado hajafanya mahojiano mpaka sasa, nipo Oysterbay kushuhudia mahojiano yake na dhamana yake,” amesema Wakili Ishabakaki.
Hata hivyo, Wakili Ishabakaki amesema hadi sasa polisi hawajaeleza rasmi tuhuma zinazomkabili Idris, ingawa kuna taarifa ya kwamba amekamatwa kufuatia kusambaa mitandaoni kwa video inayomuonesha akiicheka picha ya zamani ya Rais John Magufuli.
“Kwa ilivyo mpaka sasa hivi, hawajasema rasmi ni tuhuma gani, kwa hiyo hatuwezi kuzungumzia zaidi, lakini kwa mahojiano alivyokuwa anakutana na askari walikuwa wanazungumzia ile video aliyokuwa anacheka picha ya rais akiwa na suti ya zamani,” amesema Wakili Ishabakaki.
Leave a comment