JESHI Polisi limezidi kumpiga kalenda Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa baada ya leo tena kushindwa kumhoji na kumtaka arudi tena Alhamisi ijayo, anaandika Hamisi Mguta.
Lowassa aliwasili saa 3:05 akiwa ameambatana na Wakili wake, Peter Kibatala ambao wamekuja na msafara wa magari matatu katika ofisi ya mkurugenzi wa Upelelezi na Makosa ya Jinai, kama alivyotakiwa kufanya Juni 29.
Nusu saa baada ya kuwasili, Lowassa ameruhusiwa na kutakiwa kurudi tena Alhamisi ijayo.
Mwanasheria wa Lowassa, Peter Kibatala amezungumza na waandishi wa habari, amesema kuwa Lowassa ametakiwa kurudi Alhamisi bila sababu za kuahirishwa kwa mahojiano hayo kuwekwa wazi.
“Hatujaambiwa kwa nini ila tumeambiwa tuje alhamisi ijayo kwa ajili ya maelekezo na kuwasikiliza zaidi,” alisema.
Hii ni mara ya tatu kwa Lowassa kwenda katika ofisi za DCI ambako anahojiwa kwa tuhuma za uchochezi.
Lowassa ambaye ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, alihojiwa Juni 28 na Juni 29 na Wakili Kibatala alizungumza na wanahabari mara baada ya mahojiano hayo.
Lowassa anadaiwa kutoa maneno ya kichochezi Juni 23, mwaka huu katika futari iliyoandaliwa na mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara.
Leave a comment