Tuesday , 19 March 2024
Home Habari Mchanganyiko Polisi wafuta video ‘nyeti’ za vurugu Kinondoni
Habari Mchanganyiko

Polisi wafuta video ‘nyeti’ za vurugu Kinondoni

Spread the love

JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam lilifuta picha mnato (video), zilizochukuliwa na waandishi wa habari zikionesha askari wakiwaadhibu vikali waandamanaji wanaosadikiwa kuwa ni wafuasi wa Chadema. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).

Tukio hilo limetokea jana jioni baada ya Chadema kuhitimisha kampeni zao, uwanja wa Buibui, Kinondoni na wananchi waliohudhuria mkutano huo kuamua kutembea kuelekea Magomeni, zilipo ofisi za mkurugenzi wa manispaa ambaye ndiye msimamizi wa uchaguzi kudai fomu za viapo vya mawakala wa Chadema.

Waandishi waliokamatwa walikuwa wakirekodi video za askari wakiwapiga baadhi ya wananchi katika hekaheka za kuwatawanya wafuasi wa Chadema.

“Tulikuwa waandishi wengi akiwemo Spencer Lameck wa ITV, John Marwa wa mtandao wa Dar Mpya, Faki Sosi wa MwanaHALISI na wengineo. Polisi walipoanza kutawanya watu kwa mabomu tulipoteana, sisi wawili tukakimbilia upande wa nyuma ya magari ya polisi yaliyoweka kizuizi barabarani.

“Tukashuhudia polisi wakipiga baadhi ya watu, huku wengine wakiwa wameloana damu na mama mmoja akiwa amelala barabarani taabani, amechaniwa nguo huku akiendelea kupigwa,” amesema Charles William mmoja wa waandishi waliokamatwa.

Ameeleza kuwa alianza kurekodi video za matukio hayo kwa kutumia simu, kabla ya askari mmoja mwanamke aliyekuwa akishiriki akimpiga mama mmoja kichwani kwa kutumia fimbo alipomuona na kupiga kelele akiwataka askari wa kiume wamkimbilie na kumkamata.

“Sikutaka kukimbia kwasababu mimi si mhalifu, mimi ni mwandishi kitaaluma niliyekuwa nikitekeleza majukumu yangu. Ningekimbia lingeweza kutokea kubwa zaidi, mwenzangu Faki Sosi aliponitetea naye alikamatwa na kuunganishwa na mimi.

“Walitupiga huku wakitunyang’anya simu zetu na kusema wanahitaji neno siri ili wazione video zote zilizowaonesha wao wakipiga watu,” amesimulia.

Waandishi hao waliruhusiwa kuondoka baada ya polisi kufuta video zote za matukio ya kujeruhiwa kwa wananchi, huku polisi wakianza kuita gari ya kubeba wagonjwa (ambulance).

Imeelezwa kuwa wakati hayo yote yakitokea waandishi wengine wa habari walikuwa wamekimbilia upande mwingine ambao polisi walikuwa wakiendelea kukabiliana na wananchi waliokuwa wakiandamana.

Faki Sosi, mwandishi mwingine aliyekumbana na kashikashi za polisi amesema, “walikuwa wanamkamata Charles baada ya askari wa kike kudai amemuona akirekodi video wakati polisi wakipiga watu, sikusita kuwaambia askari kuwa huyo ni mwandishi mwenzangu anayetekeleza majukumu yake.

“Wakanikamata na mimi, walitupiga na mimi binafsi nilipigwa makofi kichwani na tukapelekwa mpaka katikati ya barabara ya mwendekosi walipopaki gari yao, walitukalisha chini barabarani na kutuamuru kutoa simu password za zimu zetu ili waone video tulizorekodi,” ameeleza.

Faki amesema askari wa kike aliyekuwa amehamaki aliwashutumu waandishi hao kuwa si wazalendo na ni mawakala wa Mange Kimambi huku askari wengine wakisema hawatawaachia wala kuwarejeshea simu kama wangekataa kutoa password.

“Tulipoona wamechachamaa tuliwapa password na wakafuta picha na video zote tulizozinasa kwenye tukio lile na wakatuachia huru huku wakitutaka tuondoke kabisa eneo lile, muda huo waandishi wenzetu ndiyo walianza kufika eneo lile.

Kimsingi tulifanyiwa uonevu mkubwa, uhuru wetu wa kikatiba na kisheria wa kuupasha umma habari umesiginwa na kupokwa kwa nguvu na vitisho vya dola,” ameeleza Faki Sosi ambaye ni mwandishi wa habari kwa miaka mitatu sasa, akiandikia gazeti la MwanaHALISI na mtandao wa MwanaHALISI Online.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari Mchanganyiko

Diwani, wananchi wengine 463 wahama Ngorongoro

Spread the loveMakamu mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro ambaye pia...

ElimuHabari Mchanganyiko

GGML yawapa mbinu wanafunzi Geita Boys kufikia malengo ya kitaaluma

Spread the loveKampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imetoa mafunzo maalumu...

Habari MchanganyikoKimataifa

Shule zafungwa kutokana na ongezeko la joto

Spread the loveSUDAN Kusini imeamuru kufungwa kwa shule zote kuanzia leo Jumatatu,...

Habari Mchanganyiko

Bunge laja na Marathon kuchangia ujenzi wa sekondari

Spread the loveBUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linatarajia kukusanya fedha...

error: Content is protected !!