JESHI la Polisi nchini Tanzania, limeeleza sababu za kuendelea kumshikilia Idris Sultani, Msanii wa Vichekesho Tanzania, anayesota rumande kwa muda wa siku tano, ni uchunguzi wa tuhuma zinazomkabili kutokamilika. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Idris anashikiliwa katika Kituo cha Polisi cha Oysterbay, wilayani Kinondoni jijini Dar es Salaam, tangu tarehe 19 Mei 2020, alipojisalimisha kituoni hapo, kwa ajili ya kuhojiwa dhidi ya kosa la uonevu kwa njia ya mtandao, linalomkabili.
Msanii huyo amekumbwa na tuhuma hizo, baada ya video inayomuonesha akiicheka picha ya zamani ya Rais John Magufuli, kusambaa mitandaoni hivi karibuni.
David Misime, Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini Tanzania, akizungumza na Mwanahalisi Online kwa simu, leo Jumamosi tarehe 23 Mei 2020, amesema msanii huyo hajapewa dhamana kwa kuwa, uchunguzi dhidi ya tuhuma zinazomkabili haujakamilika.
Misime amesema, Jeshi la Polisi haliwezi kukimbilia kumpa mtuhumiwa dhamana, wakati uchunguzi wa tuhuma zake haujakamilika.
“Kwanza niseme kwamba, ukikamatwa na polisi kwa tuhuma fulani wakati wa kukusanya ushahidi, wakati tunakuhoji tukigundua una makosa mengine tutaendelea kukuhoji nayo. Hatuwezi kukimbilia kukupa dhamana eti kwa sababu kuna dhamana,” amesema Misime
“Lazima tukamilishe haya ambayo tunaona kwamba kuna umuhimu wa kufanya uchunguzi wa kutosheleza, ili kama mtu anapoonekana kuna ushaidi wa kupelekwa mahakamani, apelekwe mahakamani na kama hakuna ushaidi aweze kuachiwa.”
Mapema leo Jumamosi asubuhi, wakati akizungumza na Mwanahalisi Online kwa njia ya simu leo, Benedict Ishabakaki, Wakili wa Idris, amesema anaendelea kufuatilia dhamana ya msanii huyo.
“Jana walikataa kutoa dhamana, na hawajatoa sababu. Wakishakwambia hakuna dhamana ina maana kesho yake unafuatilia tena, hivyo leo nafuatilia dhamana maana wanatoa siku yoyote,” amesema Wakili Ishabakaki.
Leave a comment