JESHI la Polisi Makao makuu, Ofisi ndogo Dar es Salaam limepokea lita 100 za vipukusi (sanitizers) pamoja na dispenser 5, ikiwa ni sehemu ya vifaa kinga vitavyosaidia kujikinga dhidi ya maambukizi ya homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya corona (COVID-19). Anaripoti Hamis Mguta…(endelea).
Akipokea msaada huo kutoka timu ya uhamasishaji kampeni ya “Mikono Safi, Tanzania Salama,” Kamishna wa Polisi, Kamisheni ya Uchunguzi wa Kisayansi, CP Shaban Hiki amesema, msaada huo umekuja wakati sahihi, kutokana na jeshi hilo kuwa na shughuli nyingi zinazowaweka kwenye hatari ya kupata maambukizi.”
“Jeshi la polisi lina majukumu mengi ambayo yanawaweka maafisa wake katika hatari za kupata maambukizi ya virusi vya Corona, hivyo kudai kuwa msaada huu kutoka Wizara ya Afya na Wadau wenu wa CLEAR Project umekuja wakati sahihi ” alisema.
Aidha, CP Hiki ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kuona umuhimu mkubwa wa kulisaidia jeshi hilo, hali inayoongeza kujiamini katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku ya kuwahudumia wananchi.
“Sisi msaada wenu tunauthamini sana, hata kama utakuwa mdogo kiasi gani lakini kwetu utakuwa na msaada mkubwa sana, mfano kwa wenzetu wa mikoani Mbeya na Songwe wanaenda kwenye matukio mengi sana ya mipakani, kwahiyo msaada huu kwetu ni muhimu sana” amesema.
Amesema, hata katika makao makuu uhitaji ni mkubwa sana, akitoa mfano katika kamisheni anayoongoza kumekuwa na utoaji wa hati ya tabia njema za watu wanaoomba kazi katika taasisi mbalimbali na Idara na kuwachukua vidole ili kujua uhusika wa mtu katika uharifu siku za nyuma.
Mbali na hayo, CP Hiki ametoa wito kwa wadau wengine kujitokeza kutoa msaada zaidi wa vifaa kinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona kwa jeshi hilo ili kuendelea kulilinda dhidi ya virusi hivyo.
Naye, Mkuu wa Kitengo cha maji na usafi wa mazingira, Wizara ya Afya, Anyitike Mwakitalima ameweka wazi kuwa, ugonjwa huo hauna tiba wala chanjo, huku akisisitiza kinga ndio njia pekee inayoweza kuisaidia jamii, likiwemo jeshi kupambana dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona.
“Ugonjwa huu mpaka sasa hivi hauna tiba maalum, wala chanjo, kikubwa ambacho tunatakiwa kufanya ni kuzingatia kinga, kinga ndio kila kitu kwa sasa” alisema.
Amesema, Serikali kupitia Wizara ya Afya na wadau wake itaendelea kulisaidia jeshi hilo, kwa kuendelea kugawa vifaa kinga dhidi ya maambukizi ya Corona kwa makamanda wa mikoa ili waendelea kujiandaa.
Kwa upande wake, Balozi wa kampeni ya Mikoni safi, Tanzania salama, Msanii Mrisho Mpoto (Mjomba) amesisitiza wananchi kupata taarifa kwenye vyanzo sahihi ili kuepusha upotoshaji wa taarifa ambao unaweza zua hofu na taharuki kwa wananchi.
Leave a comment