SIKU tatu baada Jeshi la Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam kuonekana wakiwaadhibu watu wenye ulemavu waliokuwa wakifanya maandamano kupinga kuzuiwa kuingia katikati ya jiji, polisi wamesema, ulemavu si kibali cha kuvunja sheria, anaandika Yasinta Francis.
Lucas Mkondya, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam amesema nguvu iliyotumiwa na polisi haikuwa kubwa na kwamba walemavu hao walifunga njia na kuvamia ofisi ya mkurugenzi wa manispaa ya Ilala na walikaidi maagizo ya jeshi hilo.
“Ulemavu si kibali cha kuvunja sheria. Hawa walemavu walifanya makosa, walivamia ofisi ya manispaa, wakafunga njia na tulipowasihi wafungue njia na wateue viongozi wa kushughulikia matatizo yao walikaidi.
“Ikabidi tutumie nguvu kidogo tu kwenda kuwaondosha. Walemavu wajaribu kuheshimu sheria za nchi kwani sheria za nchi ni lazima zisimamiwe. Polisi tukiona sheria zinavunjwa lazima tusimamie, ambaye hataki kukumbana na mkono wa polisi basi atii sheria za nchi,” amesema Kamanda Mkondya.
Amekanusha taarifa kuwa nguvu iliyotumika kuwadhibiti walemavu hao ilikuwa ni kubwa kupitiliza, pamoja na madai ya kuwepo kwa uvunjifu wa haki za binadamu.
Tukio la kukamatwa na kupigwa kwa walemavu lilitokea tarehe 16 Juni, 2017. Pamoja na mambo mengine lakini walemavu hao walikuwa wakipinga agizo la serikali la kuwataka walemavu kutoingia katikati ya jiji wakiwa na pikipiki za miguu mitatu na kuegesha katikati ya jiji.
Madai hayo ya walemavu yanalindwa na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za watu wenye Ulemavu Ibara ya 9 wa mwaka 2006.
Leave a comment