HUMPHREY Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ameeleza kuwashangaa wapinzani kwa kudhani kampeni nzuri zinaweza kuwapa ushindi. Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
“Wapinzani miaka yote hudhani ushindi katika uchaguzi hutokana na kampeni nzuri, hapana! ushindi ni matokeo ya uwekezaji wa muda mrefu ndani ya miaka mitano mliyopewa dhamana,” amesema Polepole ambaye ni mbunge aliyeteuliwa na Rais John Magufuli.
Amesema, ushindi wa chama hicho katika Uchaguzi wa Urais, Ubunge, Udiwani na Uwilishi uliofanyika tarehe 28 Oktoba 2020, umetokana na uwekezaji wa muda mrefu.
Akizungumza na wanachama wa CCM tarehe 23 Desemba 2020, jijini Mbeya, Polepole amesema uwekezaji huo umefanyika katika muhula wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Magufuli.
Katika uchaguzi uliofanyika tarehe 28 Oktoba 2020, Rais Magufuli (CCM) alipata kura 12.5, Tundu Lissu (Chadema) alipata milioni 1.9.
Pia Polepole amesema, katika uchaguzi mkuu ujao (2025) CCM kinaweza kupata asilimia kubwa zaidi ya ile ya mwaka huu katika urais.
“Sifanyi utabiri, nafanya uchambuzi, kama tukiendelea na muelekeo wa hivi 2025 ni zaidi ya asilimia 84,” amesema Polepole.
Amesema, ongezeko hilo linatokana na ushindi wa uchaguzi mkuu wa mwaka huu, ambapo CCM kimezoa wabunge, wawakilishi na madiwani wengi.
“Hatutakiwi kushuka chini ya asilimia 84 mwaka 2025, kwa sababu tukishuka wananchi watatushangaa.
“Watasema wabunge mliokuwa hamna tuliwapa, kura za urais tukawaongeza, madiwani tukawaongeza na kodi tukaongeza zaidi. Kwa nini msifanye vizuri tukawapa zaidi ya asilimia 84,” amesema Polepole.
Hata hivyo, Polepole amesema, kazi hiyo haitakuwa rahisi kama wanachama wa CCM watabweteka wakijua wamepata kila kitu.
“Lakini kazi hiyo ni ngumu sana, kwa nini? Kwa sababu kila kitu tunacho na mnapokuwa na kila kitu ndipo mtu huwa una-relax unajuna umeshamaliza, umeshapata, umeshafika,” amesema Polepole.
Leave a comment