ZANZIBAR ni ngumu. Hivi ndivyo unavyoweza kusema baada ya viongozi wa juu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuondoka patupu visiwani humo. Anaripoti Jabir Idrissa, Zanzibar … (endelea).
Mbwembwe na maneno ya kijasiri ambayo hutolewa na Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu pia Humphrey Polepole, Mwenyekiti wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho wanapopokea ‘wahamiaji,’ safari hii hazijasikika.
Licha ya Dk. Bashiru kufanya ziara visiwani Zanzibar miezi michache iliyopita na kuondoka kama alivyokwenda, Polepole naye ametoka kimya kimya Pemba.
Tayari viongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, wanaonesha shangwe kwa wakazi wa visiwa hivyo, kusimama imara bila kuhama na kujiunga na CCM kama ilivyozoeleka Tanzania Bara.
Kwa mujibu wa Salimu Bimani, Mwenyekiti wa Kamati ya Itikikadi, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma wa ACT-Wazalendo, Polepole ametoka Pemba hivi karibuni. Hakupokea mgeni yeyote.
Katika ukurasa wake wa Twitter leo tarehe 26 Februari 2020, Bimani amesema Polepole alikwenda visiwani humo kwa kishindo, lakini ameondoka kimya kimya.
“Hongera sana Mwenezi Mwenzangu Polepole, wazee wa kwetu walisema “siasa sio usheza,” umekwenda Pemba kwa kishindo umeondoka bila ya kuagwa.
“Pemba peremba Ukienda na Joho Utarudi na Kilemba” CCM Imeshakufa Pemba na Unguja,” ameandika Bimani.
Bimani ameeleza kuwa, kitendo cha Polepole kuondoka patupu Zanzibar kinaashiria kwamba, CCM imepoteza ushawishi visiwani humo.
“Mwenezi Mwenzangu mbona umeondoka Pemba kimya kimyaa!” Pemba Peremba Ukienda na Joho Utarudi na Kilemb, hivi hujui kuwa CCM imeshatalakiwa zamani Pemba na Unguja, haya kuwa uyaone. Wazee wa kwetu walisema zamani kuwa “Siasa sio Usheza.” Tukutane (Oktoba) Oct 2020 tukiwa na Tume Huru,” ameandika Bimani.
Leave a comment