MIZENGO Pinda, Waziri Mkuu Mstaafu katika Serikali ya Awamu ya Nne ameeleza kuwa, ni ndoto serikali kufikia malengo yake ya ‘serikali ya viwanda’ kama haitatekeleza mambo makuu mawili, anaandika Dany Tibason.
Amesema, kama nchi haiwezi kuwa na maji na umeme wa uhakika, haiwezekani kuwa na viwada na kufikia uchumi wa kati.
Serikali ya Awamu ya Tano imekuwa ikijinadi kuanzisha viwanda mbalimbali nchini ili kuinua uchumi wake na kusaidia wananchi, hata hivyo miongoni mwa vikwazo zinavyozungumzwa ni umeme wa uhakika, barabara na maji.
Pinda amesema ili nchi iwe katika uchumi wa kati na viwanda vidogo na vikubwa ni lazima kuwepo na maji ya kutosha na umeme wa uhakika.
Pinda ametoa kauli hiyo juzi wakati akizungumza na jumuiya ya wafanyabiashara mkoani Dodoma (TCCIA) kwa kushirikiana na ubalozi kutoka nchini India kwa lengo la kuangalia uwezekano wa kuboresha mji wa Dodoma na kuwa kitovu cha kibiashara.
Kutokana na hali hiyo Pinda amesema ili kuufanya Mji wa Dodoma kuwa kitovu cha viwanda, ni lazima kutafuta ufumbuzi wa kupata maji mengi ya kutosha na ambayo hayategemewi kutoka ardhini.
“Dodoma inaweza kuwa na viwanda vingi vidogo na vikubwa kama kutakuwa na maji ya kutosha pamoja na umeme wa uhakika.
“Hivyo basi nitumie fursa hii kuomba ubalozi wa India kusaidia kuvuta maji ya ziwa ambayo yalikuwa yaishie Singida yateremshwe hadi hapa Dodoma ili kufanikisha ujenzi wa viwanda,” amesema.
Akizungumzia umeme Pinda amesema serikali lazima iangalie namna ya kuwepo kwa umeme wa uhakika pamoja na umeme wenye bei nafuu.
Kwa upande wake mwenyekiti wa TCCIA Mkoa wa Dodoma, wakili Deus Nyabili amesema kutokana na kukosekana kwa viwanda serikali inatumia fedha nyingi kuagiza bidhaa nje.
Amesema pesa zinazotumiwa na serikali kuagiza bidhaa kutoka nje ya nchi kama zingetumika kujenga viwanda, pasingekuwepo malalamiko ya kukosa fedha kwa ajili ya kuendesha shughuli nyingine za maendeleo.
Akizungumzia suala la bidhaa zinazoletwa kutoka nje Wakili Nyabili amesema badala ya kuagiza pikipiki kutoka nchini India, ni bora viwanda vijengwe nchini.
Naye balozi kutoka India, Sandeep Arya akiwasilisha hoja kwa wadau wafanyabiashara na wajasiliamali amesema serikali ya India ipo tayari kujenga viwanda nchini hususani katika Mkoa wa Dodoma.
Mbali na hilo amesema kwa sasa wameingiza mabomba makubwa ya kutandika chini kwa lengo la kusambaza maji kwenye mji huo.
Leave a comment