KASI ya kusaka nafasi ya kuteuliwa na kugombea kiti cha urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), imedhihiri. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kauli za kushikana mashati zimeanza ‘kurushwa’, ambapo Mizengo Pinda, Waziri Mkuu Mstaafu amesema, utamaduni wa chama hicho unapaswa kuenziwa.
Pinda ambaye alichukua fomu ya kuwania urais 2015 na jina lake kuondolewa mapema, amesema wanaojipanga kuchukua nafasi hiyo kwenye uchaguzi mkuu ujao, wanajisumbua.
Kiongozi huyo mstaafu ametolea mfano tawala zilizopita kwamba, kwenye utawala wa Rais wa Awamu ya Kwanza, Pili, Tatu na Nne hakuwahi kuona haya yanayotokea sasa.
“Mimi nimefanya kazi na Mwl. Julis Nyerere kwa miaka minane, Mzee Mwinyi (Alhaj Ali Hassan), Mzee Mkapa (Rais Benjamin Mkapa) kwa miaka 10 lakini sikuona kinachojitokeza sasa,” amesema Pinda.
Akizungumza mbele ya wanaCCM jijini Dodoma tarehe 23 Julai 2019, wakati wa uzinduzi wa mradi wa vibanda vya biashara wa CCM.
Uzinduzi huo uliyohudhuriwa na Dk. Bashiru Ally, katibu mkuu wa chama hicho.
Pinda amesema, kulingana na utamaduni wa chama hicho, hakuna mwanachama wa CCM mwenye haki ya kugombea urais 2020.
Amesisitiza, Rais John Magufuli ambaye ni mwenyekiti wa chama hicho anakaribia kumaliza kipindi chake cha kwanza cha miaka mitano, hivyo ni utamaduni apewe miaka mitano mingine.
Ni kwa kuwa, utamaduni wa CCM unampa fursa rais anayetokana na chama hicho kuhudumia vipindi viwili mfululizo.
Joto la urais 2020 kupitia CCM limekolezwa baada ya Kanal Abdulrahman Kinana na Yusuf Makamba kuandika barua ya kulalamikia kufafuliwa na Cryspian Musima, anayejitambulisha kuwa mtetezi wa rais.
Maelezo ndani ya barua hiyo yametafsiriwa kuwa, ni sehemu ya njama za kumvuruga Rais Magufuli kuteuliwa na chama hicho kugombea urais 2020.
Leave a comment