MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) nchini Tanzania, imetangaza kupungua bei ya Petroli za rejareja kwa Sh.31, Dizeli ikipanda kwa Sh.9 na Mafuta ya Taa ikiongezeka kwa Sh.29. Anaripoti Brightness Boaz…(endelea)
Hii ina maana, Petroli kwa Jiji la Dar es Salaam itakuwa ikiuzwa Sh.1,834, Dizeli Sh.1,695 na mafuta ya taa Sh.1,650.
Bei ya jumla ya Petroli imepungua kwa Sh.31.10 kwa lita, wakati Dizeli ikiongezeka kwa Sh.8.74 sawa na Mafuta ya Taa Sh.29.31 kwa lita.
Bei hizo za rejareja na jumla ni kwa mafuta yaliyopokelewa kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Bei za jumla na rejareja kwa mafuta ya Petroli na Dizeli kwa Mikoa ya Kaskazini (Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara) zimebadilika.
Bei za rejareja za Petroli imeongezeka kwa Sh.31 na Dizeli ikipanda kwa Sh.61 huku bei ya mafuta ya taa zikisalia kama zilivyo.
Ewura imetoa bei hizo ambazo zinaanza kutumika leo Jumatano tarehe 6 Januari 2020.
Mikoa ya Kusini kwa maana ya Mtwara, Lindi na Ruvuma, bei zake zimebadilika ambapo Petroli imepungua kwa Sh.2, Dizeli imeongezeka kwa Sh.20.
“Mabadiliko haya ya bei yanachangiwa na kubadilika kwa bei za mafuta katika soko la dunia na gharama za usafirishaji (BPS Premium),” imesema Ewura kupitia taarifa yake kwa umma iliyotolewa na Kapwete John kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu.
John amesema, kampuni za mafuta ziko huru kuuza bidhaa za mafuta ya petroli kwa bei ya ushindani mradi tu bei hizo zisivuke bei kikomo (price cap) kama ilivyokokotolewa na kanuni (formula) iliyopitishwa na Ewura.
“Vituo vyote vya mafuta vinatakiwa kuchapisha bei za bidhaa za mafuta katika mabango yanayoonekana bayana na yakionesha bei ya mafuta, punguzo, vivutio vya biashara au promosheni zinazotolewa na kituo husika,” amesema
John amesema, wauzaji wa mafuta ya petroli wanatakiwa kutoa risiti za mauzo kutoka kwenye mashine za EFPP (Electronic Fiscal Pump Printers) na wanunuzi wahakikishe wanapata stakabadhi hizo za malipo zinazoonyesha jina la kituo, tarehe, aina ya mafuta yaliyonunuliwa na bei kwa lita.
“Stakabadhi hizo za malipo zitatumika kama kidhibiti kwa wanunuzi wa mafuta endapo kutajitokeza malalamiko ya aidha kuuziwa mafuta kwa bei ya juu kuliko bei kikomo au kuuziwa mafuta yasiyo na kiwango cha ubora kinachofaa, na pia, risiti hizo zitasaidia kurahisisha ukusanyaji wa kodi za Serikali zitokanazo na mauzo ya mafuta ya petrol,” amesema John
Bei hizo za mafuta kwa kila eneo hizi hapa chini;
Leave a comment