MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) nchini Tanzania, imetangaza ongezeko la bei ya rejareja ya petroli kwa Sh.25 na Sh.12 kwa Mafuta ya Taa kuanzia leo Jumatano tarehe 4 Novemba 2020. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Ewura imetangaza kushuka kwa bei ya Dizeli kwa Sh.44 ikihusisha mafuta hayo yaliyopokelewa kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Kwa maana hiyo, lita moja ya petrol jijini Dar es Salaam itakuwa Sh.1,902, Dizeli Sh.1,734 na mafuta ya taa itakuwa Sh.1,707.
Bei ya rejareja na jumla kwa mafuta ya petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa kwa Mikoa ya Kaskazini-Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara zimebadilika ambapo, bei ya rejareja ya petroli imeongezeka kwa Sh.52 wakati Dizeli imepungua kwa Sh.38 na Mafuta ya Taa ikipungua nayo kwa Sh.7.
Bei ya jumla ya Petroli imeongezeka kwa Sh.54.64/, wakati bei za Dizeli imepungua kwa Sh.34.64 na Mafuta ya Taa yamepungua kwa Sh.4.01.
Mabadiliko hayo yametangazwa leo Jumatano na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Godfrey Chibulunje ambaye amesema, bei za rejareja na jumla kwa bidhaa za mafuta ya Petroli na Dizeli kwa Mikoa ya Kusini- Mtwara, Lindi na Ruvuma zimebadilika.
Amesema, bei ya rejareja za Petroli imeongezeka kwa Sh.10, Dizeli imepungua kwa Sh.83 huku bei ya jumla ya Petroli imeongezeka kwa Sh.12.80 na bei ya Dizeli imepungua kwa Sh.79.67.
“Mabadiliko haya ya bei yanachangiwa na kubadilika kwa bei za mafuta katika soko la dunia na gharama za usafirishaji (BPS Premium),” amesema Chibulunje.
Amesema, kampuni za mafuta ziko huru kuuza bidhaa za mafuta ya petroli kwa bei ya ushindani mradi tu bei hizo zisivuke bei kikomo na vituo vyote vya mafuta vinatakiwa kuchapisha bei za bidhaa za mafuta katika mabango yanayoonekana bayana na yakionesha bei ya mafuta, punguzo, vivutio vya biashara au promosheni zinazotolewa na kituo husika.
“Pale ambapo inawezekana kuchagua, wateja wanashauriwa kununua bidhaa za mafuta katika vituo vinavyouza mafuta kwa bei nafuu zaidi ili kushamirisha ushindani,” amesema
Leave a comment