OFISI za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) zilizopo Mafinga, Iringa zimevamiwa. Anaripoti Bupe Mwakiteleko … (endelea).
Tukio la uvamizi huo katika Jimbo la Mbinga, limefanyika usiku wa kuamkia leo Alhamisi tarehe 10 Aprili 2019.
Akizungumza na MwanaHALISI Online, Katibu wa Chadema mkoani Iringa, Jackson Mnyawami amesema, bado haijafahamika watu waliohusika kwenye tukio hilo.
Mnyawami amesema, licha ya watu hao wasiojulikana kuvamia ofisi hizo, waliondoa bendera za chama hicho zilizoko katika maeneo ya Mbalamaziwa, Nyororo, Stendi Kuu ya Mafinga, Njiapanda ya Madibila, Ndolezi na Ifunda.
“Usiku wa kuamkia Alhamisi Aprili 10 2019, kumetokea matukio ya uvamizi wa ofisi ya chama, Jimbo la Mafinga Mjini na kuondolewa bendera.
“Kwa mfano, bendera ya Stendi Kuu Mafinga iko mita 5 kutoka Kituo cha Polisi pamoja na polisi waliopo kituoni hapo na waliopo lindo la benki ya Posta, lakini imeondolewa,” amesema na kuongeza:
“Vitendo hivi vinatokea wakati Rais John Magufuli akifanya ziara mkoani Iringa. Vitendo vya kuvamia ofisi za Chadema ni uvunjwaji wa makusudi wa Sheria ya Vyama vya Siasa, ni uporaji wa haki za vyama vyote na ubaguzi wa wazi wazi.”
Mnyawami amesema, wameliandikia Jeshi la Polisi barua ya malalamiko yao kuhusu vitendo vya kuondolewa bendera za Chadema.
“WanaCCM wanataka kumuonyesha rais kwamba Iringa hakuna Chadema, hakuna upinzani.
“Tunatoa rai kwa vyombo vya ulinzi na usalama, kuchukua hatua dhidi ya wale wote wanaohusika na vitendo hivi, kwani vinaweza kutengeneza chuki ya kisiasa na uhasama wa kisiasa hususani kwa kipindi ambacho mkoa utakuwa na ugeni mkubwa wa Rais,” amesema Mnyawami.
Leave a comment