SISTY Nyahoza, Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa nchini Tanzania amesema, Hayati Benjamin William Mkapa, Rais wa awamu ya tatu ameacha mchango wake ndani ya Chama cha Wananchi (CUF). Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza kwenye Mkutano Mkuu Maalum wa chama hicho ulioitishwa kwa ajili ya kupitisha majina ya wagombea urais Tanzania Bara na Visiwani Zanzibar leo Jumatatu tarehe 27 Julai 2020, Nyahoza amesema, miongoni mwa mambo aliyoanzisha Rais mstaafu Mkapa yaliinufaisha CUF.
Amesema, mwaka 1995, Rais Mkapa alianzisha ruzuku ya chama na kwamba, miongoni mwa vyama vya mwanzo kunufaika na ruzuku hiyo ni CUF.
“CUF ilianza kunufaika na mpango wa Rais Mkapa, lakini tulikuwa na tatizo la siasa Zanzibar, Rais Mkapa ndiye aliyesimamia na kutatua mgogoro huo kwa kusaini mkataba wa marudhiano. Sio hivyo tu, Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar uiliratibiwa na Rais Mkapa ndio maana nasema Mkapa ana historian a CUF,” amesema.
Pia, Nyahoza amesema, mpango wa Viti Maalum mwaka 2005 ulionzishwa na Rais Mkapa, CUF ni miongoni mwa vyama vya mwanzo vilivyonufaika.
Msajili huyo pia ameipongeza CUF kwa dhamira ya kufanya siasa za kistaarabu katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika tarehe 28 Oktoba 2020.
“Naipongeza CUF kwa kuamua kusimamia kauli ya kufanya kampeni kwa ustaarabu. Ninaamini mtasimamia kauli hiyo, lakini pia nampongeza Prof. Lipumba kwa kuandaa mkutano huu,” amesema Nyahoza na kuongeza “CUF bado ipo imara.”
Leave a comment