VIONGOZI watatu wandamizi ndani ya serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM), wanasuka mkakati mzito wa wizi wa kura, kwenye uchaguzi mdogo wa ubunge katika jimbo la Kinondoni. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, leo Jumapili, meneja wa kampeni wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), katika jimbo hilo, Saed Kubenea amesema, mkakati huo unasukwa kwa lengo la kumnufaisha mgombea wa CCM, Maulid Mtulia.
“Tayari tumenasa mkakati huu. Unasukwa kwa ustadi mkubwa na viongozi watatu wandamizi serikalini. Tunawaambia, waache mara moja, kwa kuwa tutakabiliana nao kwa nguvu zetu zote,” ameonya Kubenea.
Amesema, “hatuko tayari kuchezewa tena. Tumepata ushahidi mwanana unaothibitisha madai haya, tunajiandaa kuutoa hadharani ili kuwafichua wahusika.”
Uchaguzi wa ubunge katika jimbo la Kinondoni, unafanyika kufuatia Mtulia aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, kupitia Chama cha Wananchi (CUF), kutangaza kujiuzulu kwa kile alichoita, “kumuunga mkono Rais John Magufuli.”
Mtulia aliamua kujivua ubunge, tarehe 2 Desemba mwaka jana.
Kubenea anasema, katika uchaguzi huu, hakitakubali kuchezewa kama ilivyokuwa kwenye uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata 43, uliofanyika tarehe 26 Novemba mwaka jana.
“Tumejipanga kushinda na tutafanya kila liwezekanalo, kuhakikisha tunatangazwa kuwa washindi wa uchaguzi huu,” ameeleza.
Mgombea wa Chadema katika jimbo hilo, ni Salum Mwalimu; CCM imemsimamisha Mtulia, huku CUF inayotambuliwa na msajili wa vyama vya siasa, Jaji Francis Mutungi, ikiwa imemsimamisha Rajabu Salim Juma.
Leave a comment