HOSPITALI ya Rufaa ya KCMC Mkoa wa Kilimanjaro, imeanza mchakato wa ujenzi wa hosteli za wagonjwa wa saratani wenye kipato cha chini ili kuwapunguzia adha ya usafiri kutokana na baadhi yao kushindwa kumalizia matibabu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Moshi…(endelea).
Hosteli hizo zitakuwa na vitanda kati ya 45-65 zitagharimu kiasi cha dola za kimarekani 250,000 ambapo leo Ijumaa tarehe 31 Julai 202, Taasisi ya saratani ya Ohama iliyopo nchini Marekani inayomilikiwa na familia ya Dk.Luke Nordguist imekabidhi hospitali hiyo kiasi cha dola za kimarekani 100,000 kwa ajili ya kuanza ujenzi huo.
Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa hundi hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa KCMC, Dk.Gileard Masenga amesema hosteli hizo zitawasaidia kwa kiasi kikubwa wagonjwa wenye kipato cha chini kwa gharama nafuu na wale ambao hawajiwezi kabisa watasaidiwa bure.
“Hosteli hizi zitakuwa ni msaada mkubwa kwa wale wenye kipato cha chini na zitatolewa kwa gharama nafuu na wale ambao hawana uwezo kabisa watasaidiwa bure kwa kulipiwa.”
“Hatua hii itawasaidia waweze kumalizia matibabu yao, maana wagonjwa wengine huwa hawamalizi tiba zao na hii ni kutokana na pengine ugumu wa maisha hivyo tunawarahisishia,” amesema Dk.Masenga
“Mwaka jana nilikutana na familia ya Dk.Luke ambapo katika kushirikishana mawazo, tulizungumza mambo mbalimbali na alitembelea sekta yetu ya saratani na aliniahidi ataungana nasi katika kukamilisha wazo ambalo sisi tulikuwa tukilidhamiria la ujenzi wa hii hosteli kwa ajili ya wagonjwa wa saratani,” amesema
Dk. Masenga ameshukuru Mungu jana alitukabidhi dola za Marekani 100,000 kwa ajili ya kuanza ujenzi.
Dk.Luke ambaye ndio mfadhili wa ujenzi huo amesema, kipindi alipokuja Tanzania alifika katika kitengo cha saratani KCMC alikutana na Dk.Masenga na walizungumza mambo mbalimbali ikiwemo kushirikishwa wazo la ujenzi wa hosteli za wagonjwa wa Saratani hivyo akawaahidi kuwaunga mkono.
”Kutokana na kwamba nchi yetu ina mahusiano mazuri na Tanzania pamoja na hospitali hii tuliona ni jambo jema tukashirikiana ili kutatua changamoto ya wagonjwa wa saratani ambao baadhi yao wanashindwa kumalizia matibabu.”
“Leo hii mimi na kijana wangu Thomas nimekabidhi dola za kimarekani 100,000 ili ujenzi wa hosteli hii ianze mara moja,” amesema Dk.Luke
Leave a comment